Wakulima wa mahindi wazongwa na madeni kutokana na mavuno duni msimu huu
MAMIA ya wakulima wa mahindi katika Bonde la Ufa wanakabiliwa na mzigo mkubwa wa madeni baada ya ukame, uhaba wa mbolea na mashambulizi ya viwavi jeshi kuharibu mazao yao.
Hii inaweza kufanya wakulima wengi kupoteza mashamba yao yakipigwa mnada na madalali.
Kwa miaka mingi, wakulima wamekuwa wakitegemea mikopo kutoka taasisi za kifedha kufadhili kilimo wakiamini mavuno mazuri yatawasaidia kulipa madeni na kujiandaa kwa msimu unaofuata.
Lakini msimu huu hali imebadilika.
Mahindi katika eneo la Kaskazini mwa Bonde la Ufa yamekauka kabla ya kukomaa, jambo ambalo limefanya wakulima kuhofia kushindwa kulipa mikopo waliyochukua kutoka Shirika la Fedha za Kilimo (AFC), Benki ya KCB na Equity Bank.
Hofu sasa ni kuwa baadhi yao wanaweza kupokonywa mashamba na mali nyingine ikiwa watashindwa kulipa madeni yao.
Bw Samuel Macharia wa Moi’s Bridge, Kaunti ya Uasin Gishu, alisema anahangaika kutafuta namna ya kulipa mkopo wa Sh1.5 milioni aliouchukua kutoka KCB kufadhili kilimo katika shamba lake la mahindi la ekari 70.
Alisema kila mwaka amekuwa akikopa, kuvuna na kulipa mkopo bila matatizo.
Hata hivyo, ukame wa msimu huu umeharibu mazao wakati muhimu wa ukuaji.
“Kwa kawaida huwa nakopa kila mwaka na kulipa baada ya kuuza mahindi. Lakini mwaka huu mavuno yatakuwa mabaya sana na sijui nitapata wapi fedha za kulipa deni,” alisema.
Alikuwa akitarajia kuvuna zaidi ya magunia 1,500 ya mahindi na kupata zaidi ya Sh6 milioni.
Fedha hizo zingelipa mkopo na kugharimia msimu mwingine wa kilimo.
Tatizo lake limeongezeka baada ya mkewe pia kuchukua mkopo wa Sh1.2 milioni kutoka Equity Bank kununua tinga tinga.
“Tuliamini tungelipa madeni hayo kwa mapato kutoka mavuno. Lakini ukame na magonjwa ya mazao yameharibu kila kitu,” alisema.
Katika eneo la Ziwa, mkulima Michael Kosgei alisema huenda akashindwa kulipa mkopo wa Sh500,000 kutoka AFC baada ya mahindi yake ya ekari 10 kunyauka.
“Sitarajii kupata mavuno ya kutosha, hata kwa matumizi ya nyumbani. Hilo lina maana nitapata ugumu mkubwa kulipa mkopo,” alisema.
Kwa kawaida yeye huvuna kati ya magunia 25 na 30 kwa ekari lakini mwaka huu anatarajia mavuno duni sana.
Alisema wataalamu kutoka Wizara ya Kilimo walitembelea shamba lake kutathmini kiwango cha uharibifu na kukadiria mavuno yanayotarajiwa.
Wakulima wengine wanasema serikali inapaswa kuingilia kati ili kuzuia taasisi za kifedha kupiga mnada mashamba yao.
“Serikali inafaa kuwakinga wakulima dhidi ya kupoteza mashamba yao kutokana na hasara iliyosababishwa na ukame,” alisema Amos Kipchirchir wa Moiben.
Wakulima wengi Kaskazini mwa Bonde la Ufa hutegemea mikopo kununua mbegu bora, mbolea na kugharimia shughuli nyingine za kilimo.
Hata hivyo, mgogoro wa sasa umeonyesha umuhimu wa kuimarisha ufadhili wa sekta ya kilimo.
Wanamtaka Rais William Ruto kutimiza ahadi yake ya kuongezea AFC pesa kutoka Sh5 bilioni hadi Sh20 bilioni kila mwaka na kupunguza riba ya mikopo.
“Kuna mengi yanayohitajika zaidi ya mbolea ya bei nafuu. Wakulima wanahitaji mikopo ya kutosha na mabohari bora ya kuhifadhi mazao,” alisema Isaac Kosgei wa Sergoit.
Mkurugenzi Mkuu wa AFC George Kubai alisema mahitaji ya mikopo ni makubwa kuliko fedha zinazopatikana.
Alisema shirika hupokea maombi ya mikopo ya thamani ya zaidi ya Sh15 bilioni kila mwaka lakini linaweza kutoa takriban Sh4 bilioni pekee.