Habari

Mbunge wa Emurua Dikirr aonya Gachagua asikanyage Bonde la Ufa

Na VITALIS KIMUTAI August 10th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

ZIARA inayopangwa na aliyekuwa Naibu Rais Rigathi Gachagua Bonde la Ufa imezua joto la kisiasa baada ya Mbunge wa Emurua Dikirr David Keter kumwonya asithubutu kufika katika eneo hilo.

Bw Keter ambaye alichaguliwa na UDA miezi miwili iliyopita, amesema Bw Gachagua si mgeni anayekaribishwa katika eneobunge hilo.

Alirithi kiti hicho baada ya kifo cha aliyekuwa mbunge Johana Ngeno katika ajali ya helikopta Februari 28, 2026.

Onyo hilo limekuja wiki moja baada ya Kiongozi wa Wengi katika Seneti Aaron Cheruiyot kuongoza wabunge kutoka eneo hilo kusema Bw Gachagua ana uhuru wa kutembelea eneo hilo.

Hata hivyo, Bw Cheruiyot alimtaka Bw Gachagua asidhani mikutano yake itabadilika kuwa kura za DCP katika uchaguzi wa 2027.

Bw Gachagua ametangaza mara kadhaa kuwa ataanza ziara yake Kusini mwa Bonde la Ufa Bomet, Kericho na Narok kabla ya kuelekea Kaskazini mwa Bonde la Ufa ambako atatembelea Nandi, Uasin Gishu, Elgeyo Marakwet, Baringo, Trans Nzoia na Pokot Magharibi.

Baada ya Bonde la Ufa, kiongozi huyo wa DCP anatarajiwa kuelekea Magharibi kutafuta uungwaji mkono huku akilenga kulemaza umaarufu wa UDA na kampeni za Rais William Ruto.

“Nataka kumwonya Bw Gachagua asithubutu kufika Emurua Dikirr kwa sababu hakaribishwi hapa. Afadhali aelekeze nguvu zake kwingine kwani hapa ni ngome ya UDA,” akasema Bw Keter.

Katika uchaguzi mdogo wa Emurua Dikirr, Bw Keter alipata kura 18,266 na kushinda, huku mgombea wa DCP Vincent Kibet Rotich akimaliza wa pili kwa kura 10,760.

Hata hivyo, DCP imepata mafanikio katika Narok, jambo ambalo limeongeza matumaini ya Bw Gachagua kupenya ngome ya UDA.

Katika uchaguzi mdogo wa udiwani Narok Mjini mnamo Novemba 2025, mgombea wa DCP Douglas Twala Masikonte alimshinda mwaniaji wa UDA Robert Kanyinke Ole Kudate kwa kura 6,007 dhidi ya 4,479.

“Hakuna eneo la Bonde la Ufa linaloweza kugawanywa kisiasa kwa sababu watu wameelimika kuhusu haki zao. Wanaojaribu kuwazuia viongozi wa upinzani kufanya kampeni wakumbuke kuwa hawawezi kuzuia azma ya wananchi kufanya maamuzi yao,” akasema Bw Rotich.

Bw Keter pia amemshutumu Bw Gachagua kwa kuwatusi Wakalenjin huku akitafuta kura zao.

“Haikubaliki kwetu kwamba Bw Gachagua amekuwa akimshambulia Rais William Ruto na watu wa jamii yake ya Kalenjin kila siku, akiwaita majina ya kila aina kila anapopata nafasi,” akasema.

Lakini Bw Cheruiyot alisema Bonde la Ufa haiwezi kuwafungia milango viongozi wa upinzani kwa kuwa wakazi wake ni wakarimu. Seneta huyo alisema wakazi watampokea Bw Gachagua lakini wasitarajie kura.

Seneta wa Uasin Gishu Jackson Mandago pia alimkaribisha Bw Gachagua lakini akamtaka asichochee migawanyiko.

Bonde la Ufa imewahi kukumbwa na ghasia za kisiasa katika chaguzi za 1992, 1997 na 2007, ambapo mamia ya watu waliuawa, wengine kujeruhiwa na maelfu kulazimika kuyahama makazi yao.

Bw Gachagua analenga kuvutia jamii ya Kipsigis, akisema inafanana na jamii za Mlima Kenya kwa kuwa ni waaminifu lakini hawasahau viongozi wanaowasaliti.