Wantam!Macho yote kwa Gen Z iwapo watapiga kura 2027
KWA miaka mingi, vijana wamekuwa wakitajwa kuwa kundi kubwa ambalo linaweza kuamua matokeo ya uchaguzi nchini, lakini mara nyingi huwa hawapigi kura.
Hali hiyo ilibadilika mnamo 2024 wakati kizazi cha Gen Z kilipoongoza maandamano dhidi ya Mswada wa Fedha na kubadilisha kabisa ramani ya siasa nchini.
Vijana walitumia mitandao ya kijamii kama TikTok, X na Instagram kueleza kwa lugha rahisi vipengele vya Mswada wa Fedha walioamini vingeongeza mzigo wa maisha kwa Wakenya.
Kauli mbiu kama #RejectFinanceBill2024 na #OccupyParliament zilisambaa kwa kasi na kugeuza mitandao ya kijamii kuwa kituo kikuu cha kuratibu maandamano yaliyowaleta pamoja vijana kutoka maeneo na makabila mbalimbali.
Mnamo Juni 25, 2024, waandamanaji waliingia katika majengo ya Bunge wakati Mswada wa Fedha ulipokuwa ukijadiliwa, katika tukio lililovuta hisia za kimataifa. Kufuatia shinikizo hilo, Rais William Ruto aliuondoa Mswada huo na kukataa kuutia saini kuwa sheria.
Tukio hilo liliwapa vijana imani kwamba wanaweza kuathiri maamuzi ya serikali bila kutegemea vyama vya kisiasa au viongozi wa jadi.
Sasa, macho yanaelekezwa kwa uchaguzi wa 2027 na iwapo Gen Z itageuza nguvu hiyo ya maandamano kuwa nguvu ya kupiga kura.
Charles Mutisya, kijana wa Gen Z kutoka Mombasa, amesema vijana wanapaswa kuwa mstari wa mbele katika kuamua viongozi watakaoongoza nchi.
Alisema lengo ni kuwaleta pamoja makundi mengine kama waendesha bodaboda na mama mboga ili kuunda nguvu kubwa ya wapigakura.
“Tunahitaji kubaki tukiwa na umoja. Tulianzisha vuguvugu la #TukoKadi na ikiwa Gen Z tutasalia kuwa wasiojali, hatutatimiza lengo tuliloweka la kuchagua viongozi wazuri,” akasema Bw Mutisya.
Aliwataka vijana kupanga upya mikakati yao baada ya kutokea kwa migawanyiko tangu maandamano ya 2024, akisema hali hiyo imewapa wanasiasa nafasi ya kurudisha siasa za kikabila miongoni mwa vijana.
“Tunahitaji kufanya maamuzi huru 2027 kwa sababu sasa unaweza kuona wao (wanasiasa) wanatumia siasa za ukabila kutugawanya. Sitarajii Gen Z wafikiri kama mtu wa kijijini, tunahitaji kutenda tofauti na kupinga aina ya siasa tulizo nazo Kenya,” akaongeza.
Katika kampeni ya kuongeza usajili wa wapigakura iliyokamilika Aprili 2026, wapigakura wapya 2,612,725 walijiandikisha. Kati yao, 2,345,476 waliandikishwa kupitia mpango maalum wa usajili huku 267, 249 wakijiandikisha kupitia usajili wa kawaida.
Ingawa IEBC haikutoa takwimu za wapigakura hao kulingana na umri, tume hiyo ilisema vijana wengi walijitokeza, hasa kutokana na vituo vya usajili vilivyowekwa katika vyuo vya elimu ya juu.
Mnamo 2022, vijana wenye umri wa miaka 18 hadi 34 walikuwa wapigakura 8.8 milioni, sawa na karibu asilimia 40 ya wapigakura waliosajiliwa.
Gen Z wenye umri wa miaka 18 hadi 29 wanatarajiwa kuongezeka kwa kiasi kikubwa kufikia 2027, baada ya mamilioni ya waliokuwa chini ya miaka 18, 2022 kufikisha umri wa kupiga kura.
Mwanaharakati Walid Sketty wa Mombasa alisema vijana wakijitokeza kwa wingi wanaweza kuwa na kura muhimu ya maamuzi.
Kwa sasa, kushiriki kwa Gen Z katika siasa hauishii kupiga kura. Vijana wanatumia video fupi, mijadala ya moja kwa moja na mitandao ya kijamii kuelimisha wenzao, kufichua masuala ya uongozi na kuwawajibisha viongozi.
Mwenyekiti wa IEBC Erastus Ethekon alitambua nguvu hiyo baada ya zoezi la usajili wa wapigakura.
“Nyinyi ndio nguvu iliyowasha injini hii. Kupitia nyimbo zenu, lebo zenu za mitandao, dansi zenu na uhamasishaji wa rika kwa rika, mmeonyesha kuwa si viongozi wa kesho pekee, bali washikadau wakuu wa leo, na kwa kweli, mnaweza kuongoza leo,” akasema.
Huku uchaguzi wa 2027 ukikaribia, swali kuu sasa ni iwapo Gen Z itaweza kudumisha umoja wake na kugeuza ushawishi wake wa mitandao na maandamano kuwa kura.