Mbadi: Nitaendelea kuvumisha ODM na Tutam!
WAZIRI wa Fedha, John Mbadi amesema hataacha kushiriki siasa za ODM licha ya shinikizo kuwa maafisa wa serikali wajiepushe na siasa za moja kwa moja kuelekea uchaguzi wa 2027.
Bw Mbadi alisema atatumia wikendi zake kuimarisha ODM na kuhakikisha chama hicho kinapata ushindi katika uchaguzi ujao.
“Jumamosi na Jumapili zote ni siku zangu za mapumziko. Nitatumia siku hizo kushiriki siasa, hasa siasa za ODM,” akasema Bw Mbadi.
Waziri huyo, aliwahi kuwa mwenyekiti wa ODM kwa miaka 10 kabla nafasi hiyo kuchukuliwa na Gavana wa Homa Bay Gladys Wanga.
Bw Mbadi alisema ODM inaendelea kuwa na umuhimu katika siasa za Kenya licha ya vyama vingine vilivyoanzishwa baadaye kusambaratika.
Akizungumza katika hafla ya mchango eneobunge la Ndhiwa, Bw Mbadi alisema hatakaa kimya na kuacha ODM iporomoke.
Alimwahidi Bi Wanga msaada wake kuhakikisha ODM inapata zaidi ya wabunge 100 katika uchaguzi wa 2027.
“Nitakuunga mkono (Wanga) kuhakikisha ODM inapata zaidi ya wabunge 100 katika Bunge la Kitaifa. Nitatembea nawe,” akasema Bw Mbadi.
Waziri huyo alisema atashirikiana na viongozi wengine, akiwemo kiongozi wa ODM Dkt Oburu Oginga, kuhakikisha chama kinapata magavana wengi na wajumbe wengi wa mabunge ya kaunti.
“Nitawapa msaada unaohitajika pamoja na kiongozi wetu wa chama Dkt Oburu Oginga kuhakikisha ODM inapata magavana wengi na madiwani wengi katika mabunge ya kaunti. Tutafanya chochote kinachohitajika kuunga mkono ODM,” akaongeza.
Bi Wanga alisema ODM inalenga kushinda zaidi ya viti 127 vya ubunge na imeandaa mikakati ya kushinda maeneo ambayo imeyabaini kuwa na nafasi nzuri.
“Sisi kama kikosi cha ODM tuko kazini. Tuko imara tunapoelekea mbele na wakati huu tutapata zaidi ya viti 100 vya ubunge,” akasema.
Gavana huyo pia alisema ODM haitashirikiana na viongozi wanaohusishwa na aliyekuwa Naibu Rais Rigathi Gachagua, akisema chama kinaweza kujadiliana na UDA pekee.
“Ndiyo maana hatuwezi kuwa upande moja Gachagua. Anaeneza siasa za ubaguzi, siasa za makabila makubwa na madogo,” akasema.
Bw Mbadi pia alimshambulia Bw Gachagua akisema siasa za kikabila haziwezi kuwa msingi wa uongozi wa kitaifa.
“Huwezi kuwa kiongozi ambaye anaendelea kusema unataka kuwa rais kwa sababu jamii yako ina kura nyingi. Unataka kuongoza jamii yako au nchi nzima? Huyo si kiongozi ambaye tunaweza kushirikiana naye,” akasema.
Seneta Moses Kajwang alisema ODM bado ina nguvu nyingi Homa Bay na akawahimiza wakazi kujiandikisha kama wapigakura ili kuimarisha chama.
“Tunataka kujenga Kenya mpya ambako kila mtu ana haki ya kupata huduma. Ndiyo maana tulimpiga kura ya kumwondoa Gachagua. Alikuwa akisema baadhi ya mambo yamehifadhiwa kwa watu wachache na hilo si sawa,” akasema.
Seneta huyo pia aliwataka wakazi wa Nyanza kuendelea kumuunga mkono Rais Ruto, akisema serikali imeanzisha miradi ya maendeleo katika eneo hilo baada ya kifo cha Raila Odinga.
“Hatutaweza kamwe kumpa kisogo na hatuna nia ya kumfuata James Orengo au Rigathi Gachagua. Viongozi kutoka eneo hili wamekubali kufanya kazi pamoja kwa ajili ya maendeleo,” alisema.
Mbunge wa Homa Bay Mjini Peter Kaluma aliwataka wafuasi wa Linda Mwananchi kuepuka lugha ya matusi wanapopanga kuandaa mkutano wikendi ijayo.