Mahakama yapiga breki ujenzi wa msikiti Treasury Square
MAHAKAMA ya Mazingira na Ardhi mjini Mombasa imesimamisha ujenzi wa msikiti katika Bustani ya Treasury Square eneo la kihistoria na la burudani ya umma, hadi kesi iliyowasilishwa na Chama cha Wanasheria wa Mombasa itakaposikilizwa na kuamuliwa.
Chama hicho kinasema Bustani hiyo ni ardhi ya umma inayoshikiliwa kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho. Kwa mujibu wa chama hicho, mamlaka haziwezi kubadilisha matumizi ya eneo hilo bila kufuata Katiba pamoja na sheria za mipango miji na mazingira.
Mahakama imetoa amri ya muda ya kusimamisha ujenzi katika eneo hilo.
“Ombi la mlalamishi limekubaliwa. Ujenzi katika eneo hilo usitishwe hadi kesi hii itakaposikilizwa na kuamuliwa,” Mahakama iliamuru.
Mahakama pia imewaagiza washtakiwa kuwasilisha majibu yao ndani ya siku 10 baada ya kupokea hati za kesi.
Chama cha Wanasheria wa Mombasa kitapewa siku saba baada ya kupokea majibu hayo kuwasilisha kiapo cha nyongeza pamoja na hoja zake za kisheria. Washtakiwa watakuwa na siku saba zaidi kuwasilisha hoja zao.
Washtakiwa ni pamoja na Spika wa Bunge la Kaunti ya Mombasa, Aharub Khatri, Serikali ya Kaunti ya Mombasa, Tume ya Kitaifa ya Ardhi, Mamlaka ya Kitaifa ya Usimamizi wa Mazingira, Mamlaka ya Kitaifa ya Ujenzi na taasisi nyingine.
Katibu Mkuu wa Chama cha Wanasheria wa Mombasa, Natasha Ali Errey, anasema uchunguzi wa chama hicho umeonyesha kuwa ujenzi ulianza kwenye ardhi ya umma bila idhini muhimu ya kimazingira.
“NEMA ilithibitisha kuwa haikuuidhinisha ujenzi huo,” Bi Errey anasema katika hati ya kiapo ya kuunga mkono kesi hiyo.
Chama hicho kinasema ujenzi wa jengo la kudumu ulianza katika Bustani hiyo Julai 2026. Kwa mujibu wa chama hicho, jengo hilo linajengwa kwa ajili ya msikiti.
Chama hicho kinadai kuwa mradi ulianza bila wananchi kushirikishwa kikamilifu. Pia kinasema hakukuwa na mabadiliko rasmi ya matumizi ya ardhi wala vibali vyote vinavyohitajika vya mipango miji na mazingirA.
Kwa mujibu wa chama hicho, ujenzi huo umebadilisha kwa kiasi kikubwa matumizi na sura ya eneo hilo la burudani.
Pia kinadai kuwa mradi ulianza bila leseni ya tathmini ya athari kwa mazingira. Hali hiyo, kinasema, imewaweka wakazi, wafanyakazi na wageni katika hatari ya kukumbwa na vumbi, uchafu na kelele.
Chama hicho pia kinasema ujenzi huo umezuia wananchi kufikia Bustani hiyo.
Bustani hiyo ni eneo la wazi la umma lililokuwepo kwa muda mrefu. Lina ukubwa wa takriban mita 300 kwa 200 na linakabili Bunge la Kaunti ya Mombasa. Serikali ya Kaunti ya Mombasa ndilo linalolisimamia.
Bustani hiyo ni sehemu ya mandhari ya kihistoria ya Mombasa. Imezungukwa na majengo ya enzi ya ukoloni, yakiwemo Ofisi ya Kamishna wa Kaunti, Mahakama ya Rufaa na Mahakama Kuu ya Mombasa. Pia kuna maeneo mengine ya kihistoria katika mazingira yake.
Bustani hiyo ina sanamu ya shaba ya mfanyabiashara na mwanzilishi wa shughuli za elimu Allidina Visram.
Kwa vizazi vingi, Bustani hiyo imekuwa eneo la burudani, mapumziko na mikusanyiko ya umma. Miti yake mikubwa ya asili na ile iliyoletwa kutoka maeneo mengine hutoa kivuli dhidi ya joto la Mombasa. Pia huhifadhi ndege na viumbe wengine wa mijini.
“Hadi hivi karibuni, eneo hilo limetumiwa na kufurahiwa na wananchi, wakazi na wageni wa Jiji la Mombasa kama eneo la burudani, mapumziko na mikusanyiko ya umma ambako shughuli mbalimbali hufanyika,” Bi Errey anasema.
Chama hicho kinadai kuwa Bw Khatri aliongoza mradi huo akiwa katika nafasi yake binafsi na pia kama Spika wa Bunge la Kaunti. Kinasema alifanya hivyo kwa ushirikiano au kwa msaada wa walalamikiwa wengine.
Madai hayo bado hayajathibitishwa mahakamani.
Chama hicho kinataka Mahakama itamke kuwa Bustani ni ardhi ya umma inayoshikiliwa kwa niaba ya wananchi wa Mombasa na Kenya. Pia kinataka Mahakama iamuru kuwa eneo hilo haliwezi kuendelezwa bila kufuata sheria.
Aidha, kinataka Mahakama ibatilishe vibali au idhini zozote zilizotolewa kuhusiana na mradi huo na kuzuia kabisa ujenzi zaidi.
Iwapo Mahakama itaamua kuwa ujenzi huo ni kinyume cha sheria, chama hicho kinataka majengo yote yabomolewe. Pia kinataka Bustani hiyo irejeshwe katika hali yake ya awali.