Kimataifa

Raia walilia ugumu wa maisha Nigeria

Na REUTERS August 10th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

ABUJA, Nigeria

GRACE Adama huvaa hereni zake katika nyumba yake yenye vyumba viwili jijini Abuja kabla ya kuchukua mkoba na kuelekea kazini.

Mwanamke huyo anayefanya kazi katika shirika lisilo la kiserikali la afya hupokea mshahara wa Sh12,870 kwa mwezi, karibu mara mbili ya kiwango cha chini cha mshahara Nigeria.

Hata hivyo, Adama anasema maisha yanazidi kuwa magumu kwa sababu mshahara wake hauendani na kupanda kwa gharama ya maisha.

“Nikilipwa leo, mshahara wangu hudumu wiki moja tu. Gharama ya maisha, nyumba, umeme, kila kitu kimepanda,” akasema Adama.

Maisha ya mamilioni ya raia wa Nigeria yamezorota katika miaka mitatu iliyopita tangu serikali ya Rais Bola Tinubu kutekeleza mageuzi makali, yakiwemo kuondoa ruzuku ya mafuta, kushusha thamani ya naira na kupunguza ruzuku ya umeme.

Serikali na wawekezaji wanasema hatua hizo zilikuwa muhimu kuiepusha Nigeria na mgogoro mkubwa wa kifedha na hatimaye zingeleta manufaa.

Lakini kwa wananchi, gharama zimepanda.

Utafiti wa Shirika la SBM Intelligence unaonyesha gharama ya kupika mlo wa wali maarufu jollof rice imeongezeka zaidi ya mara mbili tangu Tinubu aingie madarakani.

Bei ya petroli nayo imeongezeka mara sita baada ya ruzuku kuondolewa.

Benki ya Dunia inakadiria kuwa zaidi ya nusu ya wananchi wa Nigeria waliishi katika umaskini mwaka jana, ikilinganishwa na karibu asilimia 42 mnamo 2022.

Hali hiyo inatofautiana na matumaini ya wawekezaji.

Thys Louw, meneja wa uwekezaji katika kampuni ya Ninety One, alisema wawekezaji hawajawahi kuwa na mtazamo mzuri kuhusu Nigeria kwa karibu miongo miwili.

Soko la hisa la Nigeria limepanda karibu asilimia 60 mwaka huu, huku uwekezaji wa kigeni ukifikia kiwango cha juu cha miaka sita kwa kiasi cha Sh3 trilioni mwaka jana.

Biashara na wananchi pia wanakabiliwa na mikopo ghali, huku kiwango kikuu cha riba kikiwa asilimia 26.5.

Bei ya petroli Nigeria sasa ni karibu Sh153 kwa lita, kiwango kinachowalemea wananchi waliokuwa wamezoea mafuta ya bei nafuu.

“Suluhisho kwangu ni serikali kupunguza bei ya mafuta,” alisema Eji Uchenna, muuzaji wa chakula Lagos.

Mnamo Juni, wafanyakazi wa serikali walikataa pendekezo la mshahara wa chini wa Sh9,500, wakitishia kugoma kote nchini.

Adama amesema amepunguza matumizi, kuacha nyama na kuhamia nyumba ndogo, lakini bado hulazimika kukopa ili kulipa bili.

Wakati huo huo, asilimia 80 ya raia wa Nigeria waliohojiwa na SBM Intelligence walisema nchi inaelekea upande usiofaa.

Hata hivyo, upinzani uliogawanyika unaweza kumpa Tinubu nafasi ya kushinda uchaguzi ujao.

“Serikali lazima ihakikishe ustawi unawafikia raia wote. Ukosefu wa usawa ukiendelea, hali hiyo huwa hatari,” akasema Waziri wa Fedha Taiwo Oyedele.