Habari za Kitaifa

Ruto: Kushinda ni lazima, hatuna hiari; nikifikiria jinsi nchi itakuwa mikononi mwao nashtuka

Na JOSEPH OPENDA August 11th, 2026 Kusoma ni dakika: 3

RAIS William Ruto na Kinara wa ODM Dkt Oburu Oginga jana walibuni kamati ya watu watano kutoka kila upande ili kuibuka na rasmi na manifesto ambayo watatumia kujivumisha kuelekea uchaguzi wa 2027.

Wawili hao jana waliwaambia viongozi wa Serikali Jumuishi kwamba hawana hiari ila tu kushinda Uchaguzi Mkuu 2027, huku zikibuni ushirikiano ambao utahakikisha Rais anatetea wadhifa wake.

Akizungumza jana kwenye warsha ya siku tatu ya viongozi wa muungano wa Serikali iliyofanyika Naivasha, Kaunti ya Nakuru, Rais Ruto alisema muungano mpya sio tu kwa sababu ya kuimarisha mamlaka bali kuamua mustakabali wa nchi.

Alionya kuwa ushindi wa upinzani utahujumu manufaa ambayo usimamizi wake unadai umefanikisha hadi leo.

Rais aliwahimiza viongozi wa vyama hivyo viwili kufanya kazi pamoja na kuuzia wapigakura sera yao, akisawiri upinzani kuwa usio na mpangilio na unaokosa ajenda bayana.

“Katika uchaguzi ujao ni sharti tushinde, kwa neema ya Maulana, kwa sababu hatuna hiari. Ni vigumu kutafakari kuhusu uwezekano kinyume. Inshallah, hatuna budi kushinda uchaguzi ujao sio kwa sababu yenu bali kwa maslahi ya Kenya,” akasema Rais Ruto.

Kiongozi wa nchi alisema Serikali Jumuishi ina ajenda dhahiri ya maendeleo na rekodi ya kutetea kinyume cha upinzani alioshutumu kwa kukosa maono na rekodi ya utendakazi.

“Nikiangalia chaguo mbadala ninashtuka. Kundi la watu wasio na maono wala ajenda ni hatari kwa nchi. Chaguo mbadala ni vigumu kutafakari. Upande huo ni tafrani na wanachoweza tu kufanya ni kutapatapa na kunungúnika wanapoulizwa kuhusu rekodi yao ya utendakazi,” akaongeza.

Matamshi hayo yalijiri huku Rais akiashiria kuwa uhusiano kikazi kati ya UDA, ODM huenda ukageuka kuwa muungano rasmi kabla ya kinyang’anyiro cha 2027.

Rais alisema mwongozo na ajenda ya kampeni ya muungano utajikita kwenye nakala inayotarajiwa kuibuka kutokana na warsha ya Naivasha.

Kongamano hilo lilijumuisha wabunge 250, maseneta 46, magavana 20, manaibu magavana 20 na mawaziri, akiwemo Naibu Rais Kithure Kindiki, Kinara wa Mawaziri Musalia Mudavadi, Kiongozi wa wengi katika bunge la kitaifa Kimani Ichung’wah na kiongozi wa wengi katika seneti Aaron Cheruiyot.

Rais Ruto alitaja kongamano hilo kuwa moja kati ya mikutano mikubwa zaidi ya viongozi waliochaguliwa katika historia ya nchi, na wa pili baada ya kongamano la muungano mkuu ulioandaliwa na aliyekuwa rais Mwai Kibaki na waziri mkuu wa zamani Raila Odinga.

“Si rahisi kuwaleta pamoja wabunge 250, maseneta 46 na maafisa wengine wakuu serikalini kama tulivyofanya leo. Hii inathibitisha hizi ndizo kambi mbili kubwa zaidi kisiasa nchini na ninaheshimika kuwa kinara wa moja yake,” alisema.

Rais alisema uamuzi wake kuridhiana na marehemu Raila Odinga baada ya uchaguzi 2022 ulisukumwa na hamu ya kukomesha migawanyiko kisiasa na kutafuta nyanja za kuungana kati ya kambi hizo mbili.

Alisema pande hizo mbili ziliafikiana kuhusu mipango ikiwemo nyumba za gharama nafuu, mpango wa afya kwa wote na kuimarisha uchumi.

Rais alisema kuingia kwa maafisa wa ODM serikalini kulisaidia kuharakisha utekelezaji wa ajenda yake ya uongozi, akimsifu Waziri wa fedha John Mbadi.

Dkt Oginga, aliyeongoza kongamano hilo pamoja na Rais Ruto, alitetea uamuzi wa chama chake kufanya kazi pamoja na serikali, akisema ulihitajika kuwezesha utulivu nchini na kuendeleza ajenda yake ya maendeleo.

Bw Oginga alisema ODM hapo awali iliingia kwenye mikataba kisiasa na Serikali Jumuishi lakini akahoji kuwa ushirikiano wa sasa katika ulipatia chama hicho nafasi kubwa zaidi serikalini.

“Kabla ya kujiunga na serikali, tulikuwa na ‘handisheki’ na Rais Mstaafu Uhuru Kenyatta. Hata hivyo, katika mpangilio huo hatukupata nafasi hata moja serikalini isipokuwa tu kuahidiwa kuungwa mkono kwa urais 2022,” akasema Dkt Oginga.

Bw Oginga alisema ODM ilikuwa imerejea kwenye upinzani kabla ya kujiunga na serikali ambapo wanachama kadhaa waliteuliwa katika baraza la mawaziri.

Alisema chama hicho kimejiandaa kupigia debe azma ya Rais Ruto ya kubadilisha Kenya kuwa uchumi ulioendelea duniani.

Aliwakabili vilevile viongozi wasiofurahishwa na muungano akiwataka kutangaza hadharani msimamo wao badala ya kubaki fufutende.

“Watu wazue masuala kwa ukweli, lakini usiwe fufutende. Ni sharti uamue umesimama wapi, kwa kuwa tunataka kujua ni nani yuko nasi na wale ambao hawako nasi.”

Bw Oginga alisema muungano unaandaa sera zitakazoongoza ushirikiano kuelekea uchaguzi 2027.