Maafisa wa kaunti watumia mfumo wa malipo kupora mamilioni ya pesa za umma
KAUNTI nyingi nchini zimegeuza mfumo wa malipo ya dharura maarufu kuwa njia mpya ya kupora pesa za umma kupitia madai ya matumizi yasiyo na msingi, ripoti mpya za Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali na Tume ya Maadili na Kupambana na Ufisadi (EACC) zinaonyesha.
Mfumo huu wa malipo ulianzishwa mwaka wa 2013 baada ya ugatuzi kuanza, ukiwa na lengo la kurahisisha malipo ya haraka ya matumizi madogo yasiyopangwa ambayo hayawezi kuzidi Sh2 milioni.
Lakini miaka kadhaa baadaye, mfumo huo umegeuzwa kuwa chanzo cha ufisadi huku maafisa wa kaunti wakidai fedha kwa shughuli ambazo hazikufanyika au kushindwa kuwasilisha hesabu za matumizi hayo.
Ripoti za Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali, Nancy Gathungu, na EACC zinaonyesha kuwa matumizi mabaya ya mfumo huo sasa ni mojawapo ya mbinu mpya zinazotumiwa kupora mamilioni ya pesa za walipa ushuru.
Ukaguzi wa miaka ya kifedha ya 2023/2024 na 2024/2025 umebaini kuwa kaunti huenda zilipoteza zaidi ya Sh500 milioni kupitia mfumo huo.
Katika mwaka wa kifedha wa 2023/2024 pekee, kaunti 12 zilishindwa kueleza matumizi ya zaidi ya Sh230 milioni zilizotolewa kwa malipo ya dharura.
Ripoti hiyo inaonyesha baadhi ya maafisa walipewa pesa zaidi ya mara moja, kinyume cha sheria za usimamizi wa fedha za serikali za kaunti zinazowataka kurejesha au kuwasilisha hesabu za fedha hizo ndani ya siku saba baada ya kurejea kazini.
Sheria hizo pia zinakataza afisa kupewa pesa upya kabla ya kuwasilisha hesabu ya ile ya awali au fedha hizo kukatwa kwenye mshahara wake.
Kaunti ya Turkana ndiyo inaongoza kwa fedha ambazo hazijaelezwa matumizi yake ikiwa na Sh85 milioni.
Samburu inafuata kwa Sh39.3 milioni, Mombasa Sh25.8 milioni, Bungoma Sh21.6 milioni, Tana River Sh19.8 milioni na Embu Sh12.8 milioni.
Siaya na Nandi kila moja ina Sh6.3, Kisumu Sh5.1 milioni, Nyandarua Sh3 milioni, Busia Sh1.3 milioni huku Kiambu ikiwa na zaidi ya Sh801,000.
Mkaguzi Mkuu alisema baadhi ya serikali za kaunti hazikuwa na sajili sahihi ya pesa chini ya mfumo huu kama inavyotakiwa na sheria.
Kutokana na hali hiyo, imekuwa vigumu kufuatilia nani alipokea fedha hizo, kiasi alichopewa, tarehe ya kutolewa na iwapo fedha hizo zilirejeshwa au matumizi yake kuelezwa.
Katika Kaunti ya Isiolo, ukaguzi ulibaini maafisa wawili walipewa jumla ya Sh8.4 milioni kabla ya kuwasilisha hesabu za fedha walizopewa awali.
Aidha, kaunti hiyo ilitoa Sh4 milioni kupitia kwa shughuli ya upangaji wa ardhi Garbatulla na utoaji wa hati za ugavi wa ardhi, hatua ambayo wakaguzi wanasema haikufuata utaratibu unaostahili.
Katika Kaunti ya Wajir, zaidi ya Sh149 milioni zilihamishwa kutoka akaunti za Benki Kuu ya Kenya hadi akaunti za benki ya kibiashara zilizokuwa zikitumika kwa mfumo huu na baadaye kutumiwa kwa malipo ya kawaida ya shughuli za kaunti.
Kaunti ya Embu ilikuwa na zaidi ya Sh21.8 milioni ambazo hazikuelezwa matumizi yake kufikia Juni 30, 2025.
Machakos ilikuwa na zaidi ya Sh3.6 milioni ambazo hazikuwa zimerejeshwa kwa wakati, huku Samburu ikiwa na zaidi ya Sh1.3 milioni ambazo zilikuwa zimechelewa kurejeshwa bila hatua zozote kuchukuliwa.
Katika Kaunti ya Kakamega, kulikuwa na zaidi ya Sh18.3 milioni ambazo hazikuwa zimeelezwa, huku Nandi, Uasin Gishu na Siaya zikitajwa kwa kushindwa kuweka rekodi sahihi za utoaji na urejeshaji wa fedha hizo.
Kwa upande wake, EACC ilisema imekuwa ikichunguza visa vingi ambapo mfumo huu umegeuzwa chanzo cha kujinufaisha na fedha za umma.
Mwenyekiti wa EACC, Bw Abdi Mohamud, alisema baadhi ya maafisa wamekuwa wakichukua mfumo huu kana kwamba ni pesa zao binafsi.
Ripoti hizo sasa zimeibua wasiwasi kuhusu udhaifu wa usimamizi wa fedha za umma katika kaunti na kuibua wito wa hatua kali dhidi ya maafisa wanaotumia mianya hiyo kujinufaisha kwa gharama ya walipa ushuru.