Habari

Askofu, mbunge watofautiana kuhusu mchango wa Ruto matangani

Na ANTHONY KITIMO August 15th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

IBADA ya mazishi ya marehemu Mchungaji Silvanus Mwakoma katika eneo la Kirutai, Voi, iligeuka kuwa uwanja wa malumbano ya kisiasa baada ya Mbunge wa Taveta John Bwire na Askofu Mkuu Liverson Mng’oda kutofautiana kuhusu mchango wa Rais William Ruto kwa familia ya marehemu.

Katika hotuba yake, mbunge huyo alimsifu marehemu kama mfuasi wa Rais Ruto na serikali yake.

Alitaja miradi kadhaa ya serikali katika kaunti hiyo, akisema Rais Ruto amekuwa akichangia maendeleo ya Taita-Taveta.

Bwire pia alitangaza mchango wa Sh500,000 kutoka kwa Rais Ruto, huku yeye mwenyewe akitoa Sh100,000. Hata hivyo, wakati wa mahubiri, Askofu Mng’oda alikosoa vikali kauli hizo, hasa kuhusu maendeleo ya serikali katika eneo hilo.

Askofu huyo alilalamikia hali ya barabara na ukosefu wa maji, akipinga picha ya maendeleo iliyokuwa imewasilishwa na mwanasiasa huyo.

Pia alikosoa namna mchango huo ulivyotangazwa, akidai ulitolewa kwa mtindo wa majivuno na madai ya kustahili sifa.

Katika kauli iliyowashangaza waombolezaji, Mng’oda aliishauri familia kutotumia fedha hizo kusomesha watoto wa marehemu na hata kupendekeza zirudishwe ikiwa ingewezekana.

Lakini familia haikuunga mkono msimamo huo.

Katika hotuba ya shukrani, ndugu wa marehemu aliishukuru serikali kwa mchango wa Sh500,000 na Bwire kwa Sh100,000. Alisema fedha hizo zitatumika kuwasaidia watoto wa marehemu.

Malumbano hayo yalifanya mazishi hayo kugeuka kutoka hafla ya kuaga marehemu hadi mjadala kuhusu siasa, maendeleo na matumizi ya mchango wa Sh600,000.