Jumwa aingia boksi ya Kalonzo baada ya kutema UDA
ALIYEKUWA Waziri wa Jinsia, Aisha Jumwa amejiunga rasmi na chama cha Wiper Patriotic Front, akisema yuko tayari kukabiliana na vyama vinavyounga mkono serikali jumuishi katika uchaguzi wa 2027.
Bi Jumwa alipokelewa na kiongozi wa Wiper Kalonzo Musyoka katika eneo la Kakuyuni, Kilifi, ambapo aliahidi kufanya kampeni za kuimarisha upinzani Pwani na nchini.
Hatua hiyo inatarajiwa kuongeza nguvu za Wiper katika eneo la Pwani, huku Bi Jumwa akihusishwa na mipango ya kuwania kiti cha ugavana wa Kilifi mwaka wa 2027.
Bw Musyoka alimkaribisha Bi Jumwa na kuahidi kumuunga mkono katika kinyang’anyiro hicho.
Kalonzo alisema kujiunga kwa Bi Jumwa kutaimarisha upinzani katika eneo la Pwani. Bi Jumwa alisema wakazi wa Kilifi wamechoshwa na siasa za serikali jumuishi na wanapaswa kuunga mkono upinzani.
“Hakuna tena serikali jumuishi katika Kaunti ya Kilifi kwa sababu wao ni wasaliti,” alisema.
Alisema atashirikiana na Wiper kuipaka Pwani “rangi ya samawati” kuelekea uchaguzi mkuu wa 2027.
Bw Musyoka aliwaonya viongozi wa upinzani dhidi ya kuvunja muungano wao na kujiunga na Serikali ya Kenya Kwanza, akisema hatua hiyo itakuwa usaliti kwa Wakenya wanaotaka mabadiliko katika uchaguzi wa 2027.
Bw Musyoka alisema viongozi wa upinzani lazima wabaki pamoja na kuweka kando maslahi yao binafsi wanapojenga muungano wenye nguvu wa kumkabili Rais William Ruto.
Aliwafananisha viongozi watakaoacha muungano huo na mke wa Lutu katika Biblia, ambaye aligeuka kuwa nguzo ya chumvi baada ya kugeuka nyuma licha ya kuonywa.
“Wenzangu katika upinzani… tukikubaliana na kuungana, na mmoja wetu aamue kurudi nyuma, atageuka kuwa chumvi,” alisema Kalonzo huko Kakuyuni, Kilifi.
Kalonzo alisema upinzani unahitaji kuimarisha ushawishi wake Pwani na nchini kote ili kuondoa serikali ya Kenya Kwanza madarakani.
Alisema vijana waliofikisha miaka 18 wanapaswa kupata vitambulisho na kujisajili kama wapiga kura katika zoezi la usajili wa watu wengi litakalofanyika Novemba.