Akili MaliMakala

Himizo kilimo cha kuhifadhi afya ya udongo na nishati ya jua kuunganishwa ili kupunguza gharama

Na SAMMY WAWERU August 15th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

MABADILIKO ya tabianchi yanaendelea kubadilisha kwa kasi mifumo ya kilimo nchini Kenya, huku misimu ya mvua na ukame ambayo wakulima walitegemea ikizidi kuwa isiyotabirika.

Ukame unadumu kwa muda mrefu, mvua ikichelewa au kunyesha kwa muda mfupi, huku joto linaloongezeka likiharibu rutuba ya udongo.

Wakati huohuo, gharama ya mafuta ya petroli, mbolea na pembejeo nyingine imepanda kutokana na misukosuko inayoendelea katika nchi za Milki za Kiarabu, na kufanya uzalishaji wa chakula kuwa ghali zaidi.

Wataalamu sasa wanapendekeza kuunganisha kilimo kinachofufua hadhi ya udongo, kwa Kiingereza Regenerative Agriculture (RA) na matumizi ya nishati ya jua, yaani productive use of renewable energy (PURE) katika uzalishaji ili kujenga mifumo ya chakula inayostahimili mabadiliko ya tabianchi na kupunguza uzalishaji wa gesi chafuzi.

Akizungumza katika Mkutano wa Kitaifa kuhusu Regenerative Agriculture (RA) na Productive Use of Renewable Energy (PURE) ulioandaliwa na SNV kwa ushirikiano na AGRA, majuzi, Qureish Noordin, Kiongozi wa Kiufundi wa Regenerative Agriculture AGRA, alisema afya ya udongo na nishati safi lazima viende sambamba.

Qureish Noordin, Kiongozi wa Kiufundi wa Regenerative Agriculture AGRA wakati wa mahojiano Jijini Nairobi. Picha|Sammy Waweru

Regenerative Agriculture hulenga kurejesha afya ya udongo kupitia matumizi ya mbolea zenye kaboni, mzunguko wa mazao, kilimo mseto, kilimo cha miti, nyasi za boji (mulching) na usimamizi bora wa rutuba ya udongo,” Qureish akasema.

Kwa upande mwingine, nishati ya jua inaweza kuendesha pampu za umwagiliaji mimea na maji mashamba kwa kutumia mifereji, mashine za kukausha nafaka, mashine za kupura, vifaa vya kupooza maziwa na maghala ya mifumo ya baridi, hivyo kupunguza gharama na hasara baada ya mavuno.

Utafiti wa SNV katika kaunti saba mapema kwa huu, 2026, ulionyesha kuwa gharama kubwa za teknolojia zilichangia asilimia 35 ya changamoto za matumizi, ukifuatiwa na mahitaji ya wafanyakazi kwa asilimia 22 na ukosefu wa maarifa kwa asilimia 20.

“Utafiti huo pia ulionyesha kuwa asilimia 79 ya wakulima hutumia samadi ya mifugo, asilimia 74 hulima mazao mseto, huku asilimia 73 wakifanya mzunguko wa mazao (crop rotation),” akadokeza Judith Libaisi kutoka SNV.

Hata hivyo, matumizi ya kilimo cha miti na kilimo cha kuhifadhi udongo bado ni madogo.

Judith Libaisi kutoka SNV wakati wa mahojiano Jijini Nairobi. Picha|Sammy Waweru

Libaisi alisema wakulima wanahitaji teknolojia pamoja na mafunzo ya kilimo, matengenezo, huduma baada ya mauzo na ushauri wa kitaalamu ili kupata manufaa kamili.

Kwa mkulima Esther Wariara kutoka Githunguri, Kiambu, matumizi ya pampu ya sola yamepunguza gharama za umwagiliaji kwa karibu asilimia 50, akisema sasa anatumia karibu Sh250 kwa siku badala ya Sh500.

“Kilimo hakiwezi kufanyika bila nishati,” alisema Dkt Kiplimo Lagat, Waziri wa Kilimo wa Kaunti ya Nandi, wakati wa hafla ya Regenerative Agriculture (RA) na Productive Use of Renewable Energy (PURE) iliyofanyika Jijini Nairobi Julai 2026.

Waziri huyo wa Kaunti (CEC), aidha, alisisitiza kuwa nishati safi ya jua inaweza kusaidia kuziba pengo la uzalishaji wa chakula nchini Kenya na Afrika, ikizingatiwa kuwa wakulima wanapotumia sola kupampu maji na pia kukausha mazao ili kurefusha muda wa kudumu hupunguza gharama ya uzalishaji kwa kiwango kikubwa.