Kitany arai viongozi Bondeni wachape kazi hata wakiimba TuTam
MBUNGE wa Aldai, Marianne Kitany amewataka viongozi wa UDA Bonde la Ufa kukosa kulumbana huku akisisitiza yupo tayari kumenyana na mgombeaji yeyote anayesaka ubunge.
Bi Keitany amesema kuwa rekodi yake ya maendeleo iko wazi na kwamba yupo tayari kumenyana na kiongozi yeyote lakini akasisitiza ubabe unaoendelea bondeni utatatiza kuchaguliwa kwa Rais William Ruto.
“Siasa haihusu tena kulumbana na kutusiana, inahusu kazi ambayo umefanya. Mimi naamini kwamba nitachaguliwa tena Aldai kwa sababu ya kazi ambayo nimefanya na inaonekana,” akasema Bi Kitany.
Mbunge huyo alisema yupo tayari kuwania mchujo wa UDA na mgombeaji yeyote ambaye anamezea mate kiti chake kupitia chama hicho.
“Saa hii wapinzani wangu wametoroka wote. Gavana wa sasa na mbunge wa zamani walikuwa wamesema watanipinga lakini sasa wamehepa hawana nia ya kuwania kiti hiki tena,” akasema Bi Kitany.
“Mimi niko UDA na siendi mahali popote na iwapo wanata kurudi kuwania basi niko tayari kupambana nao. Nikishindwa kwenye mchujo, sitaenda mahali popote, nitasalia tu UDA,” akaongeza.
Bi Keitany aliorodheshwa na TIFA kama mbunge ambaye ana utendakazi bora zaidi kati ya wabunge wanawake baada ya Naisula Lesuda wa Samburu Magharibi.
Bw Sang’ wiki jana alitangaza kuwa amejiondoa katika kiny’anganyiro cha ubunge baada ya kushauriana na Rais William Ruto na akimaliza muhula wake wa pili kama gavana, atakwea ngazi na kushiriki siasa za kitaifa.
Mbunge huyo anayehudumu muhula wa kwanza alimkashifu Bw Sang’ akisema utendakazi wake ni duni na hata iwapo angewania kiti hicho, hangeenda mahala popote.
“Hospitali kadhaa hazifanyi kazi, hatuna mochari ya umma inayofanya kazi. Gavana mwenyewe ana shule za chekechea ambazo bado zimejengwa kwa udongo na hata bado tunayachota maji mtoni,” akasema.
“Mengi ambayo yametimizwa yanatokana na miradi ambayo imeanzishwa na serikali kuu. Hata sasa tunakuza miwa na kuwasilisha kiwanda cha Kibos,” akasema.
Gavana Sang’ alisema kuwa hana nia ya kuwania kiti hicho cha ubunge na atamakinikia siasa za kitaifa.
“Nina hiari kuwania cheo cha kisiasa na nilikuwa niwanie useneta au niwanie ubunge Aldai. Hiari hizi ni muhimu lakini baada ya kushauriana na Rais aliniambia nimakinikie kuchaguliwa kwake 2027. Kwa hivyo, nitakuwa nashiriki siasa za kitaifa wala sitagombea cheo chochote cha kisiasa,” akasema Bw Sang’.
Mwaka jana, Bw Sang alitangaza kuwa ifikiapo 2027 atakuwa na umri wa miaka 42 ambayo ni ya chini zaidi kwa mwanasiasa kustaafu. Hii ndiyo maana sasa alikuwa akilenga kiti cha ubunge wa Aldai.
Bi Kitany alitaja kuwekwa lami kwa baadhi ya barabara, kuimarisha taasisi za elimu na kujengwa kwa masoko ya kisasa ambayo yamesaidia kuimarisha biashara katika eneobunge hilo.