Habari

Kalonzo ataka Omollo ajiuzulu, adai ameshindwa kuzima uhuni

Na CECIL ODONGO August 17th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

KIONGOZI wa Wiper, Kalonzo Musyoka amemtaka Katibu katika Wizara ya Usalama wa Ndani, Dkt Raymond Omollo kujiuzulu, akishutumu serikali kwa kushindwa kudhibiti uhuni wa kisiasa.

Bw Musyoka pia alidai kuwa ukosefu wa usalama unaoshuhudiwa katika maeneo mbalimbali ni sehemu ya mpango wa kuunda mazingira yatakayotumiwa kuahirisha Uchaguzi Mkuu wa mwaka ujao.

“Wahuni wanaeneza hofu na hatuwezi kufuata mkondo huo. Katibu Omollo lazima ajiuzulu kwa sababu mkuu wake amekataa kumtimua ilhali kuna visa vya ukosefu wa usalama kila mahali,” akasema Bw Musyoka alipokuwa akizungumza katika Kanisa la Reedemed Gospel Kithimani, Kaunti ya Machakos.

Alishangaa kwa nini vitendo vya kihuni vinaendelea licha ya Rais William Ruto kutoa hakikisho hapo awali kwamba serikali ilikuwa imemaliza tatizo hilo.

Bw Musyoka alitaja ghasia zilizoshuhudiwa Homa Bay Jumapili, ambapo waandishi wawili wa habari walijeruhiwa na biashara kufungwa kuelekea mkutano wa Linda Mwananchi.

Pia alirejelea vurugu zilizotokea katika eneobunge la Rongai Kaunti ya Nakuru Jumamosi, ambapo msafara wa aliyekuwa Naibu Rais Rigathi Gachagua ulipigwa mawe na mikutano ya kisiasa kuvurugwa.

Bw Musyoka pia alielekeza lawama zake kwa Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC), akisema Wakenya wanafuatilia kwa karibu kila hatua inayochukuliwa katika maandalizi ya Uchaguzi Mkuu wa 2027.

“IEBC inapaswa kuwaruhusu Wakenya kuwachagua viongozi ambao hawajatwaliwa na serikali. Tulisema hatuwezi kuelekea katika uchaguzi ujao tukiwa na Smartmatic kama kampuni inayotoa programu ya uchaguzi, na tunajua michezo hii na lazima ikome,” alisema.

Bw Musyoka aliandamana na Gavana wa Machakos Wavinya Ndeti, Mwenyekiti wa Wiper na aliyekuwa Mbunge wa Kigumo Jamleck Kamau, Seneta wa Machakos Agnes Kavindu na Naibu Gavana Francis Mwangangi.

Bw Kamau alimuunga mkono Bw Musyoka katika azma yake ya kuwania urais 2027, akisema ana ushawishi wa kitaifa nje ya Ukambani.

“Kalonzo si mwanasiasa wa Wakamba pekee, yeye ndiye rais wa sita wa Kenya. Kuanzia wikendi ijayo tutaanza ziara zetu za kisiasa na haki itakuwa msingi katika chama hiki,” alisema Bw Kamau.

“Kalonzo ni mtu wa amani na 2007, kama hangeungana na Mwai Kibaki, nchi isingekuwa na amani. Amejitolea kwa dhati kwa Raila na sasa ni zamu yake. Hana doa. Ikiwa tunataka kiongozi mwenye amani, basi huyo ni Kalonzo Musyoka,” akaongeza Bw Kamau.

Bw Musyoka pia alizungumzia utata wa bajeti katika Bunge la Kaunti ya Machakos, akiwataka MCA kuidhinisha bajeti hiyo ili serikali ya kaunti iweze kuendelea kutoa huduma kwa wananchi.

“Bajeti si pesa za kibinafsi za gavana, kwa hivyo tushirikiane na tusonge mbele,” akasema kiongozi huyo wa Wiper.

Gavana Ndeti alimtaka Rais Ruto na vyombo vya usalama kuchukua hatua madhubuti dhidi ya vitendo vya kihuni na kurejesha usalama nchini.

Pia alimuunga mkono Bw Musyoka kuwania urais 2027, huku akiwakosoa madiwani kwa kuidhinisha nusu tu ya bajeti ya kaunti, ambayo alisema inaweza kugharamia mishahara pekee.

“Bila bajeti hatuwezi kutoa huduma ambazo wananchi wetu wanahitaji. Nimewaita madiwani ili tukae pamoja kwa sababu ni sisi tutakaoipeleka kaunti hii mbele,” alisema Bi Ndeti.