Dimba

Mashabiki kuingia bure kushuhudia mechi kati ya Kenya Junior Starlets na Bantwana ya Afrika Kusini

Na TOTO AREGE July 10th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

Mashabiki wa soka wataingia bure kushuhudia mechi ya marudiano kati ya Kenya Junior Starlets na Bantwana ya Afrika Kusini katika raundi ya mwisho ya kufuzu Kombe la Dunia la Wanawake la wachezaji chini ya miaka 17, itakayopigwa Jumapili katika Uwanja wa Nyayo, Nairobi.

Mchezo huo utaanza saa tisa alasiri, huku mashabiki watakaoketi kwenye sehemu za kawaida wakiruhusiwa kuingia bila malipo. Wale watakaotaka huduma za VIP watalazimika kununua tiketi kwa Sh500.

Mshindi wa jumla baada ya mechi mbili atajinyakulia tiketi ya mwisho ya Afrika kushiriki Kombe la Dunia la Wanawake la U17 litakalofanyika Morocco kuanzia Oktoba 17 hadi Novemba 8.

Kenya inaingia katika mechi hiyo ikiwa na faida kubwa baada ya kuibuka na ushindi wa mabao 2-0 dhidi ya Afrika Kusini katika mechi ya mkondo wa kwanza iliyochezwa Lucas Moripe Stadium, Pretoria, Jumamosi iliyopita.

Kiungo mshambuliaji Faith Boke ndiye aliyefungua ukurasa wa mabao dakika ya 13 kabla ya mshambuliaji Brenda Achieng kuongeza la pili dakika ya 70 na kuiweka Kenya katika nafasi nzuri ya kutinga michuano hiyo kwa mara ya pili katika historia.

Kocha Mildred Cheche na kikosi chake wanahitaji sare ya aina yoyote.

Kwa upande mwingine, Bantwana chini ya kocha Ntombifuthi Khumalo wanahitaji ushindi wa mabao matatu bila kuruhusu bao ili kugeuza matokeo na kunyakua tiketi ya kwenda Morocco.

Kikosi cha Afrika Kusini kiliwasili Nairobi Alhamisi jioni na kilitarajiwa kufanya mazoezi yake ya kwanza Ijumaa asubuhi kabla ya kufanya mazoezi ya kuuzoea Uwanja wa Nyayo Jumamosi jioni.

Historia pia iko upande wa Junior Starlets, ambao hawajawahi kupoteza nyumbani baada ya kushinda mechi ya kwanza ugenini katika mechi za kufuzu Kombe la Dunia.

Kocha Cheche na wachezaji wake watakuwa wakilenga kuepuka machungu ya mwaka jana, ambapo Kenya ilikosa tiketi ya Kombe la Dunia baada ya kuondolewa na Cameroon katika hatua ya mwisho ya kufuzu.

Starlets walipoteza 3-1 mjini Yaounde kabla ya kupigwa 1-0 katika mechi ya marudiano ugani Nyayo, matokeo yaliyokatiza ndoto zao za kurejea katika jukwaa la dunia baada ya kucheza kwa mara ya kwanza 2024 nchini Jamhuri ya Dominica.