Habari za Kitaifa

Raia saba wa Amerika walioshukiwa kuwa na Ebola waondoka Karantini Laikipia

Na MERCY CHELANGAT August 18th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

WAFANYAKAZI saba raia wa Amerika kutoka Shirika la misaada la Samaritan’s Purse wameachiliwa kutoka kituo cha kuwatenga wagonjwa wa Ebola cha Laikipia Air Base baada ya kukamilisha siku 21 za karantini.

Walikuwa chini ya uangalizi kama tahadhari walipokuwa wakisaidia shughuli za kukabili visa vya dharura katika eneo hilo. Mkurugenzi wa Samaritan’s Purse Kenya, Alex Kuria, alisema wote hawakuonyesha dalili zozote za Ebola na sasa wamerejea nyumbani.

“Watu hao wameondoka na kurejea nyumbani. Wamekuwa nyumbani kwa wiki mbili sasa wala hawakuonyesha dalili zozote. Walikuwa salama na hakuna wengine wapya waliofika,” akasema.

Wafanyakazi hao walikuwa sehemu ya kikosi cha Amerika cha kukabiliana na majanga na waliishi katika mahema maalumu ya kijeshi kwenye kituo hicho.

Kuachiliwa kwao kunafanyika wakati Kenya ikiimarisha maandalizi kukabili mkurupuko wa Ebola katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC) na maeneo ya jirani.

Kenya bado haijathibitisha kisa chochote cha Ebola. Hadi sasa, wasafiri 413,017 wamepimwa katika vituo vya kuingia nchini, huku sampuli zote 196 zilizochunguzwa zikiwa hazina virusi.

Wizara ya Afya imezindua maabara tano za Ebola, zikiwemo mbili katika vituo vya mpakani vya Busia na Lwakhakha.

Pia kuna sehemu za kuwatenga wagonjwa ambazo zimeandaliwa katika hospitali kadhaa, zikiwemo Hospitali ya Kenyatta, Hospitali ya Police, ile ya Rufaa ya Mafunzo ya Moi na Port Reitz.

Mkurugenzi Mkuu wa Afya, Dkt Patrick Amoth, amesema Ebola bado ni tishio kwa Kenya kutokana na nafasi yake kama kitovu cha usafiri kwenye ukanda huu.

“Ebola bado ni tatizo la afya ya umma. Hali nchini Congo bado ni mbaya japo Uganda imefanikiwa kudhibiti mkurupuko, lakini kwa sababu sisi ni kitovu cha usafiri kati yetu, DRC na eneo hili, tumeweka mifumo ya kukabiliana na mkurupuko iwapo utafika nchini,” akasema.

Alisema Kenya imechunguza zaidi ya watu 183 na wote walipatikana bila virusi.

Dkt Amoth alisema kiwango cha maandalizi ya Kenya kimeongezeka kutoka asilimia 66 hadi 88 kulingana na tathmini ya Shirika la Afya Duniani (WHO).

“Tunataka kuwahakikishia Wakenya kwamba tumeweka mifumo inayohitajika kuzuia, kugundua na kukabiliana ipasavyo na ugonjwa huu,” akasema.

Hata hivyo, ripoti ilionyesha kuwa vituo 23 vya afya katika kaunti zilizo hatarini vinahitaji kuboreshwa ili kufikia viwango vya WHO.

Kufikia Agosti 12, jumla ya visa 4,665 vya Ebola vilikuwa vimethibitishwa DRC, Uganda na Ufaransa, huku watu 2,184 wakifariki, kulingana na Kituo cha Kudhibiti magonjwa ya Kuambukizana (CDC) Amerika.