Habari za Kitaifa

Gachagua awasilisha rufaa ya kurasa 121 kupinga kutimuliwa kwake

Na JOSEPH WANGUI August 18th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

ALIYEKUWA Naibu Rais Rigathi Gachagua jana aliwasilisha rufaa katika Mahakama ya Rufaa kupinga uamuzi wa Mahakama Kuu uliothibitisha kuondolewa kwake mamlakani na Seneti mnamo 2024.

Rufaa hiyo, yenye kurasa 121, inapinga uamuzi wa Juni 8, 2026 uliotolewa na Majaji Eric Ogola, Anthony Mrima na Frida Mugambi.

Miongoni mwa hoja kuu ni madai kwamba Mahakama Kuu “ilibadilisha uamuzi wa mwisho wa maandishi na kuufanya kutofautiana na uamuzi uliotolewa hadharani mahakamani.”

Bw Gachagua anadai vifungu vinne vilivyosomwa baada ya aya za 484, 488, 503 na 508 viliondolewa katika uamuzi wa maandishi licha ya kusomwa hadharani na kupeperushwa moja kwa moja kwenye runinga.

“Kwa kubadilisha uamuzi isivyofaa, mahakama imemnyima hoja nzito za mahakama zilizotolewa katika vifungu vilivyosomwa baada ya aya za 484, 488, 503 na 508,” akasema.

Pia anapinga uamuzi wa Mahakama Kuu wa kuunga mkono kuondolewa kwake licha ya majaji kubaini kuwa Seneti ilikiuka haki zake za kikatiba wakati wa mchakato huo.

Majaji walibaini kuwa haki yake ya kusikilizwa na kuchukuliwa hatua za kiutawala ilikiukwa baada ya Seneti kukataa kuahirisha kikao alipougua na kushindwa kukamilisha utetezi wake.

Bw Gachagua anasema ukiukaji huo ulipaswa kufanya uamuzi wa Seneti kuwa usiofaa.

“Mahakama Kuu ilikosea kimsingi kisheria kwa kushindwa kubaini kwamba uamuzi wa Seneti wa kumuondoa mamlakani ulikuwa batili na usio na nguvu za kisheria,” akasema.

Anapinga pia msimamo kwamba uamuzi wa Seneti kuhusu kutimuliwa kwake hauwezi kuchunguzwa na mahakama, akisema mahakama zinaweza kuingilia mchakato huo iwapo Katiba imekiukwa.

Pia anasema mahakama ilikosea kuzingatia hoja ya uwezekano wa kuwepo kwa Naibu Rais wawili iwapo angewarejeshwa mamlakani, kwani alikuwa amebadilisha ombi lake na hakutaka kurudi ofisini bali alitaka kutimuliwa kwake kubatilishwe na apewe fidia.

Pia anapinga mchakato wa Seneti, akisema uchunguzi ulikuwa wa lazima na kamati maalum ilipaswa kuundwa.

Ushirikishaji wa umma ni hoja nyingine. Bw Gachagua anasema Seneti haikuwashirikisha wananchi baada ya kupokea ripoti ya Bunge la Kitaifa.

Pia anapinga mchakato wa uteuzi na kuidhinishwa kwa Kithure Kindiki kuwa Naibu Rais.

Zaidi ya hayo, anasema mahakama ilishindwa kuamua kuhusu haki yake ya kulipwa hela za kustaafu. Anapinga fidia ya Sh50 milioni, akisema haikutosha.

Bw Gachagua anaiomba Mahakama ya Rufaa itangaze uamuzi wa Seneti wa Oktoba 17, 2024 kuwa kinyume cha Katiba, batili na usiokuwa na nguvu za kisheria.