Msichana ahadithia jinsi baba humdhalilisha kingono kabla kumpa mahitaji ya shule
MAHAKAMA ya Eldoret ilipigwa na butwaa Jumatatu wakati msichana mwenye umri wa miaka 16 alipoeleza jinsi baba yake mzazi alivyomdhulumu kingono mara kwa mara kila alipokuwa akimuuliza mahitaji ya shule.
Msichana huyo, aliyetambuliwa kwa jina la siri A.W., alisimulia masaibu yake kwa majonzi kwa kukariri madhila aliyopitia mikononi mwa babake mzazi A. W wakati wa kusikizwa kwa kesi hiyo mahakamani.
Akiwasilisha ushahidi wake mbele ya hakimu mkuu mkaazi Keyne Gweno, alieleza kuwa baada ya mama yake kufariki dunia na kuwaacha mabinti wanne akiwemo yeye, waliendelea kuishi chini ya uangalizi wa baba yao.
“Wakati wowote mwalimu wangu aliponiambia nilete kitabu na kalamu, kadri nilipomwomba baba yangu aninunulie vitu hivyo ndivyo alinilazimu kushiriki naye tendo la ngono kabla ya kuninunulia vitu husika,” alisimulia.
Mahakama ilielezwa kuwa licha ya kutishiwa maisha iwapo angefichua unyama huo, hatimaye msichana huyo aliamua kumweleza mmoja wa walimu wake kuhusu unyanyasaji aliokuwa akifanyiwa.
Walimu kutoka shule hiyo walichukua jukumu la kutoa ripoti kwa polisi ambapo mshukiwa alikamatwa na maafisa wa polisi kutoka kituo cha polisi cha Langas na kufikishwa katika mahakama ya Eldoret.
Mwanaume huyo alifikishwa mahakamani na kushtakiwa kwa kosa la kufanya tendo la ngono na mtu wa familia ya karibu yaani kujamiiana, kinyume na Kifungu cha 20 (1) cha Sheria ya Makosa ya Kijinsia Nambari 3 ya mwaka 2006.
Hati ya mashtaka inaeleza kuwa katika tarehe mbalimbali kati ya Januari 16, 2026, na Februari 6, 2026, katika eneo la Lemmok katika Kaunti Ndogo ya Kapseret, Kaunti ya Uasin Gishu, alimdhulumu kimapenzi binti yake mwenye umri wa miaka 16 kwa makusudi na kinyume cha sheria.
Hata hivyo, mshtakiwa alikana mashtaka hayo kabla ya kuamrishwa kuwachiliwa kwa dhamana ya Sh300,000 au dhamana mbadala ya pesa taslimu kiasi cha Sh100,000.
Tangu wakati huo, mshtakiwa ambaye alishindwa kupata pesa taslimu za dhamana au dhamana ambapo amezuiliwa katika rumande ya Gereza la Eldoret GK akisubiri kesi kusikilizwa kikamilifu na kuamuliwa.
Ombil la kutaka kupunguziwa dhamana ya pesa taslimu kutoka Sh100,000 hadi Sh50,000 lilikataliwa mahakamani.
“Sitapunguza zaidi kiasi hicho cha dhamana ya pesa taslimu cha Sh100,000 kwa sababu najua kuwa mara tu utakapopata uhuru wako, hutawahi kurejea mahakamani hapa,” aliamuru Hakimu.
Akitoa ushahidi kuhusu suala hilo, Dkt Irene Simiyu, daktari katika Hospitali ya Rufaa na Mafunzo ya Moi (MTRH), alithibitisha kuwa binti huyo alikuwa amedhulumiwa kingono.
Upande wa mashtaka umepanga kuwasislihsa mashahidi watano muhimu, akiwemo afisa upelelezi kutoka Kituo cha Polisi cha Langas.
Kesi hiyo iliahirishwa hadi Septemba 8, 2026.