TAHARIRI: Gavana Ayacko awajibishwe kuhusiana na matamshi yake
MATAMSHI ya Gavana wa Migori Ochilo Ayacko kuhusu ziara inayopangwa ya Gavana wa Siaya James Orengo na viongozi wengine wa vuguvugu la Linda Mwananchi yanatia wasiwasi na yanastahili kulaaniwa vikali.
Kauli hii imetolewa wiki moja tu baada ya ghasia za kisiasa katika Kaunti ya Homa Bay kusababisha vifo vya watu wawili na kujeruhiwa kwa wengine kadhaa.
Kenya inahitaji viongozi wa kisiasa kupunguza joto la kisiasa, kuheshimu Katiba na kulinda haki ya kila raia kushiriki katika shughuli za kisiasa kwa amani.
Badala yake, Bw Ayacko ametoa matamshi ambayo yanaweza kuongeza hofu na kutoa taswira kwamba ghasia dhidi ya wapinzani wa kisiasa zinafaa kuvumiliwa.
Kauli yake kwamba “kuna jambo linaweza kumfanyikia Orengo” ni uchochezi.
Gavana si mwanasiasa wa kawaida tu. Yeye ni afisa mkuu wa umma ambaye maneno yake yana uzito na yanaweza kuwachochea wafuasi wake na viongozi.
Iwapo Bw Ayacko anaamini kweli kwamba kuna tishio la kiusalama dhidi ya Bw Orengo au kiongozi mwengine yeyote, wajibu wake uko wazi.
Anapaswa kuripoti suala hilo kwa vyombo husika vya usalama na kudai ulinzi wa kutosha. Hapaswi kutoa kauli zisizoeleweka kuhusu kile kinachoweza kumtokea mwanasiasa mwenzake.
Katiba ya Kenya inahakikisha uhuru wa kutembea, kujumuika, kukusanyika na kushiriki katika shughuli za kisiasa.
Hakuna gavana, afisa wa chama au kiongozi wa eneo anayepaswa kujiona kuwa na mamlaka ya kuamua ni nani anayeruhusiwa kutembelea kaunti fulani, kuzungumza na wakazi au kutafuta uungwaji mkono wa kisiasa.
Bw Orengo hahitaji mwaliko kutoka kwa wanasiasa wa Migori ili kutembelea kaunti hiyo, mradi shughuli zake zinafanywa kwa mujibu wa sheria.
Matukio ya kusikitisha ya Homa Bay yalipaswa kuwafundisha viongozi wa kisiasa kuhusu heshima.
Kabla ya ghasia za Agosti 16, kulikuwa na matamshi makali ya kisiasa. Matokeo yake yalikuwa fujo, maafa, majeruhi na kuharibiwa kwa mali.
Afisa mmoja wa polisi na mfanyabiashara mwanamke walifariki, huku wakazi wasio na hatia wakibaki kuhesabu hasara za mzozo wa kisiasa ambao haukupaswa kuruhusiwa kugeuka kuwa vurugu.
Mashindano ya kisiasa kuelekea Uchaguzi Mkuu wa 2027 hayaepukiki lakini vurugu zinaepukika.
Viongozi wanaweza kutofautiana vikali kuhusu mustakabali wa ODM, serikali ya Rais William Ruto na mwelekeo wa kisiasa wa eneo la Nyanza bila kugeuza miji na vijiji kuwa viwanja vya machafuko.