Nchimbi agusia Samia katika sababu za kujiuzulu: ‘Nimeona Rais anatamani mabadiliko’
DAR ES SALAAM, Tanzania:
MAKAMU wa Rais wa Tanzania, Dkt Emmanuel John Nchimbi, Jumanne, Agosti 25, 2026 alitangaza uamuzi wake wa kujiuzulu wadhifa wake na kustaafu kabisa katika utumishi wa umma na siasa kuanzia Septemba 4, 2026.
Katika taarifa rasmi kwa umma iliyotolewa na Afisi ya Makamu wa Rais jijini Dodoma, Dkt Nchimbi alisema tayari amemkabidhi Rais Samia Suluhu Hassan barua rasmi ya kujiuzulu.
Dkt Nchimbi alisema ameongozwa na masharti ya Ibara ya 50(2)(c), na Ibara ya 149(2) ya Katiba ya Tanzania, ili kumpa Rais Hassan fursa ya kumteua makamu wa rais mwingine.
Akikumbuka kipindi chake cha uongozi, Dkt Nchimbi alisema alikuwa ametoa ahadi kwa rais mwaka mmoja uliopita kwamba angeitumikia Tanzania kwa uaminifu na kuwa tayari kuondoka iwapo kungekuwa na haja ya mabadiliko.
“Mnamo Agosti 27, 2025, nilimuahidi Mheshimiwa Rais Dkt Samia Suluhu Hassan kwamba ningemsaidia yeye na nchi yetu kwa uwezo wangu wote na kwa uaminifu mkubwa,” akasema Dkt Nchimbi.
“Pia nilimhakikishia kwamba wakati wowote atakapoona kuna haja ya kuwa na makamu wa rais mwengine, nitaachia wadhifa huo. Nimeridhika kabisa, bila shaka yoyote, kwamba Rais anatamani mabadiliko, na kwa hivyo nimeamua kutimiza ahadi yangu,” akasema
Dkt Nchimbi alimshukuru Rais Hassan na chama tawala, CCM, kwa imani waliyoonyesha katika uongozi wake.
Pia aliwashukuru raia wa Tanzania kwa kumuunga mkono katika kipindi chake cha utumishi wa umma, akiahidi kuendelea kuwa raia mzalendo.
Kujiuzulu kwake hata hivyo pia huenda kunatarajiwa kuzua maoni ya kisiasa hasa baada ya Tanzania kuwa na uchaguzi mkuu uliopita uliozingirwa na utata na kukosolewa na jamii ya kimataifa.
Dkt Emmanuel John Nchimbi alizaliwa Desemba 24, 1971, katika Mkoa wa Mbeya na alilewa katika familia iliyojikita katika utumishi wa umma.
Babake, Mzee John Nchimbi, ambaye anatoka Wilaya ya Songea, aliwahi kuhudumu kama Kamishina Msaidizi wa Polisi na Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Mtwara.
Mbali na kazi yake katika idara ya polisi, Mzee Nchimbi pia alijihusisha na siasa, akihudumu kwa mihula miwili kama mwanachama wa Kamati Kuu ya Taifa ya CCM kupitia tawi la majeshi, kabla ya baadaye kuhudumu kama katibu wa chama hicho katika ngazi ya mkoa.