Habari za Kaunti

Ndovu wanaharibu mazao shambani kwangu Taveta, Rais Ruto alalamika

Na WINNIE ATIENO August 26th, 2026 Kusoma ni dakika: 3

RAIS William Ruto amefichua kuwa ndovu wamekuwa wakivamia shamba lake lililoko Taita-Taveta na kuharibu mimea licha ya juhudi za kuwazuia, huku mizozo kati ya binadamu na wanyamapori ikizidi kutishia jamii katika eneo la Pwani.

Rais alisema ndovu waliingia katika shamba lake na kuharibu mimea yake ya mahindi pamoja na kuangusha ua wa umeme aliokuwa ameweka kulinda mimea yake dhidi ya uvamizi huo.

Alisema kuwa anafahamu changamoto zinazowakabili wakulima wanaoishi karibu na mbuga za wanyamapori.

“Mimi pia ninakabiliwa na uvamizi wa ndovu katika shamba langu. Wamekula na kuharibu mimea yangu ya mahindi; pia nimepata hasara. Nilijaribu kuweka ua wa umeme lakini waliuvunja na kuendelea kula na kuharibu mimea yangu,” alisema Rais Jumapili wakati wa ibada kanisani katika kaunti hiyo.

Hata hivyo, Dkt Ruto, ambaye anafuga ng’ombe wa nyama na maziwa katika shamba hilo pamoja na kuendesha kilimo cha mboga, alisema amewasiliana na Shirika la Huduma kwa Wanyamapori nchini (KWS) kutafuta suluhu ya kudumu.

“Lazima tupate suluhu ya kudumu kupitia mitaro na uzio ili kuwazuia wasiingie katika mashamba yetu,” alisema.

Mbunge Mwakilishi wa Kike Taita-Taveta, Bi Lydia Haika, alisema uvamizi wa ndovu ni tatizo kubwa katika kaunti hiyo na kumtaka Rais kutafuta suluhisho ya kudumu.

Haya yanajiri huku maelfu ya wakulima katika jamii zinazoishi karibu na hifadhi za kitaifa za Tsavo Mashariki na Tsavo Magharibi, wakiendelea kulalamika kuhusu uvamizi wa wanyamapori katika mashamba na makazi wakitafuta chakula na maji.

Katika kaunti za Kilifi, Kwale, Taita-Taveta, Lamu na Tana River, wakazi wameripoti uharibifu wa mimea, mali na vitisho kwa usalama wao kutokana na wanyamapori.

Hivi majuzi mwanafunzi wa Gredi ya Saba alishambuliwa na kuuawa na simba Machi 29 alipokuwa akirejea nyumbani kutoka shuleni katika Kaunti ya Kilifi.

Tukio hilo liliwalazimu maafisa wa KWS kuwasindikiza wanafunzi kwenda na kutoka shuleni katika baadhi ya vijiji vilivyoathirika.

Hali imekuwa mbaya zaidi eneo la Ganze, ambako wakazi wanasema ndovu wamekuwa wakiingia mara kwa mara katika mashamba na makazi.

Miezi minne iliyopita, zaidi ya ndovu 300 waliripotiwa kutoka katika Hifadhi ya Kitaifa ya Tsavo na kuvamia vijiji vya Kilifi, wakiharibu mimea, vyanzo vya maji na mashamba, ikiwemo mali ya Katibu Mkuu wa Idara ya Masuala ya Vijana, Bw Fikirini Jacobs.

Uvamizi huo ulizua hasira na huku wakazi wakitoa wito kwa serikali kujenga uwa wa umeme kuzunguka hifadhi ya kitaifa ya Tsavo ili kuwazuia wanyamapori kuingia katika maeneo ya makazi.

Katika kaunti jirani ya Kwale, Mbunge wa Kinango, Bw Gonzi Rai, alimuomba Rais Ruto kuingilia kati akisema ndovu wamekuwa wakiharibu mimea na kuzidisha ukosefu wa chakula.

“Tafadhali tusaidie kutatua tatizo hili. Ndovu wanaharibu mimea yetu na ndiyo maana wakazi wanategemea misaada ya chakula kila mara. Hatutaki kutegemea misaada kwa sababu sisi ni wakulima. Changamoto pekee tunayokabili ni uvamizi wa ndovu ambao wanaendelea kuharibu mashamba yetu,” alisema Bw Rai.

Hivi majuzi, Naibu Kamishna wa Magarini, kaunti ya Kilifi, Bw Michael Ololtuaa pia alilitaka Shirika la Huduma kwa Wanyamapori nchini (KWS) kujitahidi na kuhakikisha kila mwaathiriwa wa migogoro ya binadamu na wanyamapori anafidiwa kikamilifu.

Katika mahojiano na Taifa Leo Jumapili, Bw Ololtuaa alisisitiza kuwa si jambo jema kuona mwaathiriwa wa wanyamapori akikosa kufidiwa kutokana na kufeli kwake kusajili matukio kwa KWS.

Kumekuwa na visa vya wanyamapori, hasa simba kuvamia, kuwaua na kuwala wanafunzi eneo hilo la Magarini.

Kisa cha hivi punde zaidi ni cha juma lililopita ambapo simba-jike alimvamia,kumuua na kumla mwanafunzi wa Gredi 4 katika kijiji cha Chanjalo, Magarini, kaunti ya Kilifi.

Mwanafunzi huyo kwa jina Kelvin Amani alikuwa njiani kurudi nyumbani jioni baada ya kucheza mpira wakati alipovamiwa na simba huyo.

Machi, 2026, mwanafunzi mwingine wa Gredi 7 kwa jina Simon Nzaro Chai, kutoka kijiji cha Watala, eneobunge la Magarini, pia alivamiwa na kuliwa na simba wakati akitoka shule.

Katika ziara yake ya awali huko Kilifi, Rais Ruto alitangaza kuwa serikali ilikuwa imetenga Sh315 milioni kujenga uzio wa umeme wenye urefu wa kilomita 140 kuzunguka hifadhi hiyo.

“Nimesikia changamoto mnazokabiliana nazo kuhusu mzozo kati ya binadamu na wanyamapori. Hili lilizungumzwa pia na Gavana Gideon Mung’aro, Mbunge wa Ganze Kenneth Tungule na viongozi wengine. Nilikuwa nimeahidi kutafuta fedha na sasa nimepata Sh315 milioni za kujenga uzio wa umeme wa kilomita 140 kuzunguka hifadhi ya kitaifa,” alisema wakati wa hafla ya shukrani ya Bw Jacobs.

Rais alisema uwa huo unalenga kuzuia ndovu na wanyamapori wengine kutoka katika hifadhi na kuingia kwenye mashamba na vijiji.

“Tunajua kila mnapopanda mimea, wanyama wa porini huja na kuiharibu. Lakini tatizo hili litakwisha mwaka huu na hali ya kawaida itarejea. Hili ndilo ninawaahidi,” alisema.

Rais Ruto pia alisema Mkurugenzi Mkuu wa KWS Prof Erustus Kanga, alikuwa akikamilisha mchakato wa zabuni na kwamba wakandarasi walitarajiwa kuanza kazi kufikia Julai.