Wanafamilia 6 wapatikana na hatia ya kuua jamaa waliyeshuku alimroga mtoto aliyeugua
WATU sita wa familia moja wamepatikana na hatia ya kumuua mmoja wao baada ya kumshuku kuwa alihusika na ugonjwa wa ajabu uliompata mmoja wa watoto wa familia hiyo.
Kalume Ngonyo Mwavuo, Kadenge Ngala, Abdalla Ponda, Ramma Ngonyo, Simon Kaingu na Mwalimu Karisa walipatikana na hatia ya kumuua Kazungu Magogo Mwavuo mnamo Julai 2, 2024, katika kijiji cha Lutsangani, Kaunti ya Kilifi.
Mahakama Kuu ya Mombasa ilibaini kuwa sita hao walishiriki kwa pamoja katika shambulio lililosababisha kifo cha Kazungu baada ya familia kumshuku kuwa alitumia uchawi kumsababishia Nassir Mumba Hoto, mwanawe Mwavuo, kuugua.
“Kwa hivyo, mahakama inapata kila mmoja wa washtakiwa sita na hatia ya kosa la mauaji,” mahakama ilisema katika uamuzi uliotolewa Julai 24.
Kwa mujibu wa ushahidi uliowasilishwa mahakamani, Nassir aliugua ghafla na hali yake ikazua hofu miongoni mwa ndugu zake.
Familia ilianza kumshuku Kazungu, mjomba wa Nassir, kuwa ndiye aliyesababisha ugonjwa huo kwa njia za kishirikina.
Kazungu aliitwa kutoka nyumbani kwake na kupelekwa katika makazi ya Mwavuo, ambako Nassir alikuwa akiugua.
Familia ilijaribu kumtaka Kazungu kusaidia kuondoa hali hiyo waliyoamini ilikuwa imempata Nassir. Hata hivyo, juhudi hizo ziliposhindikana, hali ilibadilika na kuwa ya vurugu.
Kazungu alipigwa na kufanikiwa kutoroka hadi kwa jirani akitafuta usalama. Hata hivyo, washambuliaji wake walimfuata na kuendelea kumpiga hadi alipoanguka.
Baadaye alifariki kutokana na majeraha aliyopata.
Binti wa Kazungu aliieleza mahakama kuwa baadhi ya washtakiwa walifika nyumbani kwao majira ya saa tisa alasiri na kumwambia baba yake kuwa kaka yake alikuwa mgonjwa na alihitaji msaada wake.
Alimwona babake akiondoka pamoja nao kuelekea kwa Mwavuo. Akiwa hapo, alishuhudia Ponda akimpiga babake kwa jembe huku mtu mwingine akimshikilia.
Kakake pia alitoa ushahidi wa kumuunga mkono, akisema Mwavuo na Ponda walishiriki katika kumpiga Kazungu.
Ushahidi huo uliungwa mkono na jirani, Karisa Kazungu, ambaye alisema aliamshwa na kelele wakati wa usiku na kumwona Mwavuo na Ngala wakimshambulia Kazungu.
“Niliwaona Mwavuo akimpiga marehemu nyuma ya kichwa na Ngala pia akimshambulia,” alisema.
Daktari Ruth Nyangi, aliyefanya uchunguzi wa mwili wa marehemu, aliambia mahakama kuwa Kazungu alikuwa na majeraha kadhaa kichwani, michubuko na majeraha mengine mwilini.
Alisema marehemu alikuwa na fuvu lililovunjika, damu iliyovuja ndani ya utando wa ubongo na majeraha ya ubongo.
Daktari huyo alihitimisha kuwa Kazungu alifariki kutokana na jeraha kubwa la kichwa lililosababishwa na kupigwa na kifaa butu.
Washtakiwa wote sita walikana kuhusika na mauaji hayo, ingawa walikiri kuwepo katika makazi hayo wakati Kazungu aliitwa.
Mwavuo alisema alikuwepo lakini hakushiriki katika shambulio hilo.
Ngala alisema alitoka nje baada ya kusikia kelele, huku Ponda akikiri kuwa Kazungu aliitwa kutokana na ugonjwa wa Nassir lakini akakana kuona shambulio hilo.
Ramma alisema familia ilikuwa imejaribu kumfanyia Nassir taratibu za kumwondolea hali hiyo kabla wazee kutoridhishwa na matokeo.
Hata hivyo, alikana kushiriki katika mauaji. Kaingu na Karisa pia walikana kuhusika. Mahakama hata hivyo ilisema ushahidi uliotolewa uliwaunganisha sita hao na matukio yaliyosababisha kifo cha Kazungu.
Jaji alibaini kuwa wote walikuwa pamoja katika makazi hayo, walishiriki katika kumwita Kazungu na walikuwepo wakati hali ilipogeuka kuwa ya vurugu.
“Washukiwa walitenda kosa hilo kwa nia ya pamoja, mazingira ya shambulio pamoja na ukubwa wa majeraha yaliyosababisha kifo yalithibitisha nia ovu ya kuua,” alisema Jaji huyo.
Sita hao wataendelea kuzuiliwa huku wakisubiri kutoa malilio yao kabla ya kuhukumiwa.
Vile vile, Mahakama imeagiza pia kuandaliwa kwa ripoti za kabla ya hukumu na taarifa ya madhara yaliyosababishwa kwa familia ya marehemu ili kusaidia katika kuamua adhabu inayofaa.
Kesi hiyo itarejea mahakamani Septemba 30.