Sare baada ya sare: Wakuu wa usalama watetea mavazi mapya ya polisi
MAAFISA wa polisi nchini wataanza kuvalia sare mpya kuanzia Ijumaa na kutelekeza ile ya rangi ya samawati iliyozinduliwa wakati wa utawala wa Rais mstaafu Uhuru Kenyatta.
Sare hizo mpya zitachukua nafasi ya sare za sasa zinazovaliwa na maafisa wa polisi wa kawaida, huku Polisi wa Utawala (APS) na Kitengo cha Kupambana na Ghasia (GSU) wakitarajiwa kuendelea kutumia sare zao za sasa.
Inspekta Jenerali wa Polisi Douglas Kanja alisema mabadiliko hayo yamekumbatiwa baada ya malalamishi ya polisi kuhusu mavazi ya sasa.
“Tumeitumia sare ya rangi ya samawati iliyokolea, kwa hivyo sasa tumerudi kwenye ile tuliyokubaliana. Ninataka pia kubainisha kuwa Jumatatu nami nitakuwa nimeivaa hiyo sare mpya,” akasema Bw Kanja.
Inspekta Jenerali huyo alizungumza Jumanne baada ya kuhudhuria gwaride la mazoezi la polisi wa cheo cha konstebo waliokuwa wakipata mafunzo katika Chuo cha Polisi cha Kiganjo, Kaunti ya Nyeri. Alisema polisi wanaotarajiwa kuhitimu Ijumaa watakuwa wa kwanza kuvalia sare hizo mpya.

Rais William Ruto anatarajiwa kuzindua rasmi sare hizo katika Chuo cha Polisi cha Kenya wakati wa hafla ya kuhitimu kwa polisi 10,000 wa cheo cha konstebo, ambao baadaye watajiunga na idara ya polisi.
Bw Kanja alisema hatua ya kubadilisha sare inalenga kuinua ari ya maafisa na kuboresha utoaji wa huduma kwa wananchi.
Mabadiliko hayo yanajiri kufuatia zoezi la ushirikishaji wa umma lililofanyika 2023, ambapo maafisa wengi wa polisi walikataa sare za sasa za samawati iliyokolea na kutaka zibadilishwe ili ziwe za starehe zaidi na zinazostahili mahitaji ya kazi yao.
Mnamo 2018, Huduma ya Kitaifa ya Polisi (NPS) ilianzisha sare za sasa za rangi ya samawati kama sehemu ya ajenda ya mageuzi katika idara ya polisi.
Hata hivyo, muundo huo wa rangi, haukupokelewa vyema na baadhi ya maafisa. Wengine walidai kuwa sare hizo hazikuwa za starehe wala za kuvutia.
Baadhi yao hata walizilinganisha na mavazi yanayovaliwa na wanakwaya makanisani.
Lakini hatua ya serikali ya Rais Ruto kuanzisha sare mpya inaibua maswali kuhusu mapendekezo yaliyotolewa na Jopo la Kuangazia Mageuzi ya Polisi aliyekuwa Jaji Mkuu David Maraga.
Jopo hilo lilipendekeza polisi wavae sare zao za zamani kwa muda wa miaka mitatu huku mchakato wa kubuni sare mpya ukianzishwa kwa kufuata mapendekezo yaliyomo katika ripoti yake.
“Kuhusu sare za NPS, kwa kuzingatia maoni mengi ya wananchi, maafisa wa polisi wenyewe na uongozi wa NPS, jopo linapendekeza NPS irejee kwa sare zake za zamani kwa kipindi cha miaka mitatu. Baada ya mchakato wa kubuni sare mpya utaanzishwa kwa mujibu wa mapendekezo katika ripoti hii,” ikasema ripoti hiyo.
Ripoti hiyo pia ilipendekeza kuanzishwa kwa Kamati ya Kitaifa ya Sare, ambayo ingejumuisha wawakilishi kutoka huduma mbalimbali za usalama na taasisi za maafisa wanaovaa sare.
Kulingana na mapendekezo hayo, Waziri wa Ulinzi, kwa kushauriana na Waziri wa Usalama wa Ndani, angeandaa sheria ya kuanzisha kamati hiyo yenye jukumu la kuidhinisha viwango, rangi na ubora wa sare zinazotumiwa na kila huduma.
“Kamati hiyo inapaswa pia kushughulikia matumizi mabaya ya sare na wananchi,” ripoti hiyo ilisema.
Mbali na sare, ripoti ya jopo hilo ilibaini mapungufu katika usimamizi wa rasilimali za polisi.
Ilibaini kuwa huduma hizo hazikuwa zimeweka kikamilifu mifumo yao ya rasilimali watu katika mfumo wa kidijitali, hali ambayo imekuwa ikizua mianya ya udanganyifu, ufisadi na matumizi mabaya ya mamlaka.
Pia, baadhi ya kazi za rasilimali watu zinafanywa na maafisa wenye sare ambao hawana mafunzo ya kitaalamu katika usimamizi wa wafanyakazi, jambo ambalo limechangia makosa katika masuala ya kiutawala.
Jopo hilo lilipendekeza kuwa, isipokuwa masuala ya kiutendaji yanayohusu kupelekwa kwa maafisa katika maeneo mbalimbali, kazi nyingine zote za rasilimali watu zisimamiwe na wataalamu wenye mafunzo, tajriba na uwezo unaohitajika.
“Uwekaji kamili wa huduma zote za rasilimali watu katika mfumo wa kidijitali, ikiwa ni pamoja na malipo ya marupurupu, utahakikisha mahitaji ya maafisa wote wa NPS yanashughulikiwa kwa haraka,” ripoti hiyo ilisema.