Habari

Siasa: IEBC yapiga breki kampeni katika maeneo ya ibada, mazishini

Na SAMWEL OWINO August 22nd, 2026 Kusoma ni dakika: 2

TUME Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC) imewapa wanasiasa na wanaowania nyadhifa mbalimbali waliochapisha mabango ya kampeni yenye nembo ya tume hiyo siku tano kuyaondoa mara moja, ikiongeza juhudi za kukabiliana na kampeni za mapema kuelekea Uchaguzi Mkuu wa Agosti 10, 2027.

Katika taarifa kuhusu maandalizi ya uchaguzi huo, IEBC ilisema matumizi ya nembo yake kwenye vifaa vya kampeni ni kinyume cha sheria na yanaweza kutoa taswira ya kuunga mkono wagombeaji fulani, jambo linalohatarisha uhuru, kutopendelea upande wowote na hadhi yake kama taasisi isiyoegemea siasa.

“Tume imebaini matumizi yasiyoidhinishwa ya nembo yake kwenye vifaa vya kampeni. Matumizi hayo si halali na yanaweza kuashiria kuwa tume inaunga mkono wagombeaji husika,” ilisema IEBC.

Tume hiyo ilionya kwamba yeyote atakayeshindwa kuondoa vifaa hivyo ndani ya siku tano atachukuliwa hatua za kisheria.

Ingawa wanasiasa wengi wamekuwa wakizuru maeneo mbalimbali nchini wakitafuta uungwaji mkono, IEBC imesisitiza kuwa kipindi rasmi cha kampeni bado hakijaanza. Kwa mujibu wa sheria, kampeni za uchaguzi wa 2027 zitaanza baada ya mgombeaji kuidhinishwa rasmi na tume, lakini si kabla ya Mei 29, 2027, na zitakoma Agosti 7, 2027, saa 48 kabla ya siku ya kupiga kura.

Tume ilisema kuwa kuonyesha mabango, kutumia misafara ya kampeni, mabango makubwa ya matangazo na njia nyingine za kushawishi wapigakura kabla ya muda uliowekwa ni kinyume cha sheria.

Aidha, IEBC imeonya dhidi ya matumizi ya makanisa, misikiti na mazishi kama majukwaa ya kampeni. Tume ilisema itaweka kikamilifu Kanuni ya Maadili ya Uchaguzi ili kuwachukulia hatua wote watakaokiuka masharti hayo.

“Watu wote wanaofungwa na Kanuni ya Maadili ya Uchaguzi wanapaswa kujiepusha na kampeni katika maeneo ya ibada na wakati wa mazishi,” ilisema.

IEBC iliongeza kuwa kuvunja kanuni hizo kunaweza kufanya wahusika kuzuiwa kushiriki uchaguzi unaojiri au hata uchaguzi wa baadaye.

Pale ambapo kutakuwa na vurugu, vitisho au ukiukaji mkubwa wa sheria, tume inaweza kuwasilisha kesi katika Mahakama Kuu kupata amri inayofaa.

Kuhusu ongezeko la makundi ya wahuni katika mikutano ya kisiasa, IEBC ilisema inafanya kazi kwa ushirikiano na idara za usalama na haki ili kuhakikisha uchaguzi wa 2027 unafanyika kwa mazingira ya amani.

Tume pia ilikumbusha kuwa maafisa wa umma wanaonuia kugombea uchaguzi huo lazima wawe wamejiuzulu kufikia Februari 10, 2027.