Habari za Kitaifa

Benki ya KCB yadai kuna njama ya kuilaghai Sh146 bilioni

Na JOSEPH WANGUI August 26th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

BENKI ya KCB imepiga ripoti kwa DCI ikitaka ichunguze kampuni ya Foxcapital inayodai ilituma Sh146 bilioni kwenye akaunti yake kutoka ng’ambo kuhusiana na uwekezaji wa dhamana za serikali.

Benki hiyo inadai kwamba stakabadhi zilizowasilishwa na kampuni hiyo kortini kudai fedha hizo ni ghushi na inataka DCI kubaini ni nani aliziandaa, kusambaza na kuziwasilisha kortini.

Mzozo unahusisha €978,675,835 (Sh146.3 billion), ambazo Foxcapital inasema ilituma kwa akaunti yao ya KCB Oktoba mwaka jana kama malipo kwa kampuni ya Uingereza, Bay Bionics Ltd, iliyotambuliwa zamani kama BB Biotech AG Limited.

Foxcapital iliwasilisha kesi mapema mwezi huu ikidai kwamba KCB ilipokea fedha hizo za kigeni lakini ikakosa kuziweka kwenye akaunti yake, na kufanya Mahakama Kuu kubana hela hizo ikisubiri iamuliwe iwapo benki hiyo kweli ilipokea pesa hizo na kukataa kuzipeana kwa kampuni husika.

Katika kilio chake kwa DCI kitengo cha Ulaghai wa Benki, KCB Group, kupitia Afisa Mkuu Mtendaji Paul Russo anatilia shaka stakabadhi zilizotumiwa na Foxcapital kudai pesa hizo.

Stakabadhi zinajumuisha arafa za SWIFT, ripoti ya tukio ya Aprili 17, barua ya Mei 18 ya kuangazia kosa la kiuchumi na utathmini wa kiufundi wa Julai 1.

KCB inasema stakabadhi zinazodaiwa kutoka UBS Switzerland AG na maafisa wa KCB sio halisi.

Kulingana na malalamishi hayo, KCB iliandikia UBS Agosti 13, 2026 ikitaka thibitisho la stakabadhi na malipo.

KCB inasema UBS ilijibu ikisema stakabadhi na maagizo ya malipo “hayajatoka kwa UBS Switzerland AG na kwa hivyo sio halali.”

KCB inasema inatilia shaka stakabadhi hizo baada ya kupata kwamba hakuna mtiririko wa malipo kama hayo kutoka kwenye mitambo yao.

“Ikichukuliwa kwa pamoja, kukosekama kwa malipo hayo kwenye mitambo yetu, UBS Switzerland AG kukana stakabadhi na kiapo cha Ushahidi kutoka kwa maafisa wa KCB pamoja na stakabadhi za kutiliwa shaka kunaipa KCB kuamini kwamba kuna njama ya kuilaghai Sh146 bilioni inayoendeshwa na Foxcapital,” KCB inasema.

  • Imetafsiriwa kutoka Business Daily na Fatuma Bariki