Aliyejifanya padri na kuongoza misa kadhaa Turkana ndani
MWANAUME anayeshtakiwa kwa kujifanya padri wa Kanisa Katoliki aliingia katika shughuli za Jimbo Katoliki la Lodwar, kuongoza misa pamoja na Askofu John Mbinda na baadaye kuongoza ibada katika makanisa kadhaa kabla ya kutiliwa shaka.
Mshukiwa huyo, Jones Bogonko Onchonga, sasa amezua maswali katika Jimbo la Kanisa Katoliki la Lodwar kuhusu jinsi alivyoweza kutekeleza majukumu ya kasisi bila kuwa na mamlaka hayo.
Mnamo Agosti 16, 2026, jimbo hilo lilitoa taarifa likiwaonya mapadri na waumini kuwa Bw Onchonga si padri wa Kanisa Katoliki.
“Rev Fr Jones Bogonko Onchonga, M.C si padri wa Kanisa Katoliki. Kwa hakika, yeye ni mwanamume aliyeoa mwenye watoto wawili huko Kisii,” ilisema taarifa iliyotiwa saini na Askofu Mbinda.
Jimbo lilimlaumu Bw Onchonga kwa kukiuka sheria kadhaa za Kanisa Katoliki, ikiwemo kujifanya kutoa sakramenti, kuendesha ibada bila ruhusa na kutumia nyaraka za kanisa kwa njia isiyo halali.
Alifikishwa mbele ya Hakimu Mkuu Evanson Ngigi mjini Lodwar Agosti 14 na kukiri shtaka la kujifanya mtu mwingine kinyume na kifungu cha 382 cha Sheria ya Adhabu.
Hata hivyo, alibadilisha msimamo huo Agosti 17 mbele ya Hakimu Michael Lokitam.
Inadaiwa kuwa kati ya Julai 31 na Agosti 12 alitumia udanganyifu kumshawishi Askofu Mbinda na viongozi wa jimbo kwamba alikuwa padri aliyeteuliwa na aliyepewa mamlaka ya kuendesha shughuli za kanisa.
Kwa sasa anazuiliwa katika Gereza la GK Lodwar baada ya kukosa dhamana ya Sh100,000 pamoja na mdhamini wa kiwango hicho, au dhamana ya pesa taslimu ya Sh50,000
Kabla ya kutiliwa shaka, Bw Onchonga alikuwa tayari amepata nafasi ndani ya jimbo hilo.
Mnamo Agosti 5, aliungana na Askofu Mbinda kama mmoja wa mapadre walioshiriki misa katika Kanisa Kuu la St Augustine wakati wa uzinduzi wa Legion of Mary.
Baada ya misa, Askofu Mbinda aliondoka kuelekea Nairobi huku Bw Onchonga akiendelea kuongoza misa nyingine.
Mnamo Agosti 9, waumini katika Shrine ya St Mary’s, Lodaraja, karibu na Mto Kawalase, walianza kumtilia shaka.
Akiwa amevalia vazi la kasisi la kijani, alidai kuwa alikuwa na uhusiano wa kifamilia na Askofu Mbinda.
Waumini walisema alionekana kuchanganyikiwa wakati wa kuendesha misa.
Picha yake akiendesha ibada ilisambazwa katika kundi la WhatsApp la mapadre na askofu, na kusababisha maswali zaidi kuhusu utambulisho wake.
Mpelelezi mmoja alisema Bw Onchonga wakati fulani alijaribu kumpa muumini sakramenti ambayo haikuwa imetakaswa.
Akihojiwa katika ofisi za DCI Lodwar, Bw Onchonga alisema aliwahi kukutana na Askofu Mbinda katika Chuo Kikuu cha Tangaza na alitaka kuwasiliana naye tena baada ya kuondoka Tanzania.
Sasa jimbo hilo linakabiliwa na maswali kuhusu taratibu za kuthibitisha watu wanaohudumu kama mapadre na iwapo mtu yeyote ndani ya kanisa alimsaidia mshukiwa huyo kupata nafasi hiyo.