Shangazi Akujibu

Mke aliniambia hasikii mdundo wa ngoma, sasa naogopa hata kumkaribia!

Na SHANGAZI AKUJIBU August 27th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

NILISHANGAA sana mke wangu kuniambia simridhishi kimapenzi. Badala ya kukasirika, nilihuzunika sana na nikaanza kujiona sitoshi mboga. Tangu siku hiyo nimekuwa nikiepuka hata kuanzisha ukaribu kwa sababu naogopa kukataliwa tena. Yeye sasa anasema hakukusudia kuniumiza, alitaka tu tuzungumze kuhusu kile ambacho kila mmoja anahitaji. Tatizo ni kwamba mimi nimeanza kujitenga kihisia. Nifanyeje?

Mazungumzo kuhusu ngono na ukaribu yanaweza kuwa magumu kwa sababu yanagusa hisia za mtu kuhusu mwili na kujiamini. Lakini kueleza mahitaji hakumaanishi mwenzako anakudharau. Jaribu kuona mazungumzo hayo kama nafasi ya kujifunza kuhusu mwenzako, si mtihani wa kuwa mwanamume. Muulize kwa heshima ni mambo gani angependa yabadilike, na wewe pia eleza mahitaji yako.

Amehepa baada ya kunipachika mimba

Tangu mpenzi wangu anipachike mimba, amejitenga sana. Hashiki simu zangu wala kujibu SMS ninazomtumia. Sijui nifanye nini.

Kujitenga kwake baada ya mimba ni dalili ya kutowajibika. Jaribu mazungumzo ya moja kwa moja ili kupata msimamo wake. Akikwepa bado, anza kuangalia maisha yako ya baadaye dada.

Wanataka tumfurushe mama, tuuze boma halafu sisi watoto tugawane pesa

Baba aliaga miaka miwili iliyopita na alituachia nyumba ambayo sisi ndugu watano tunamiliki kwa pamoja. Wanne wanataka tuiuze tugawane pesa. Mimi nimekataa kwa sababu hiyo ndiyo nyumba tulikulia na mama bado anaishi humo. Ndugu zangu wanasema ninazuia maendeleo yao. Mama naye hataki kuondoka kwa sababu kila kona ya nyumba ina kumbukumbu za baba. Sasa tumekuwa tukigombana kuhusu mali hiyo. Nifanyeje?

Hisia na masuala ya urithi mara nyingi huchanganya, hivyo ni muhimu kutenganisha thamani ya kihisia na haki za kisheria. Ikiwa mali iko katika umiliki wa pamoja, maamuzi yake yanapaswa kufanywa kwa kufuata taratibu zinazofaa. Jambo muhimu ni kutomfukuza mama bila mpango wa makazi salama. Pia epukeni vitisho na ugomvi wa kifamilia. Mali inaweza kugawanywa, lakini uhusiano wa ndugu ukivunjika, si rahisi kuurekebisha.

Maisha ya wengine mtandaoni yanipa presha, nifanyeje nipate utulivu?

Marafiki zangu wanaposti jinsi wanavyofanikiwa kimaisha na hii inanipa presha sana. Inafanya nihisi kushindwa na maisha. Nifanyeje?

Maisha si mashindano, kila mtu ana safari yake. Sherehekea na ujivunie mafanikio yako madogo. Uko sawa, usijipe presha