Habari

Wabunge waliochaguliwa kwa tikiti huru wataka kuwa na usemi bungeni

Na SAMWEL OWINO August 29th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

ABUNGE watakaochaguliwa kwa tiketi huru katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2027 huenda wakapata kiongozi wao rasmi katika Bunge la Taifa pamoja na ofisi inayofadhiliwa na walipakodi, iwapo mapendekezo ya marekebisho ya Kanuni za Kudumu za Bunge yatapitishwa.

Katika barua iliyoelekezwa kwa Spika wa Bunge la Taifa, Moses Wetang’ula, wabunge hao huru wanataka kiongozi wao awe na ofisi, sawa na ilivyo kwa viongozi wa walio wengi na walio wachache bungeni.

“Spika anaweza, kufuatia ombi la maandishi kutoka kwa angalau wabunge huru 10, kutambua rasmi kundi la wabunge huru kwa madhumuni ya kuwawezesha kutekeleza wajibu wao katika Bunge la Taifa,” inasema sehemu ya barua hiyo.

Barua hiyo, iliyotiwa saini na Mbunge wa Kisumu Mashariki Shakeel Shabbir, ambaye ni mwenyekiti wa kundi la wabunge huru, pia inapendekeza marekebisho ya Kanuni ya Kudumu nambari 259(1) ili kujumuisha kiti maalum kilichotengwa kwa kiongozi wa wabunge huru.

“Kutakuwa na viti maalum ndani ya ukumbi wa Bunge kwa matumizi ya kipekee ya Naibu Spika, Kiongozi wa Chama cha Walio Wengi, Kiongozi wa Chama cha Walio Wachache, wabunge wenye ulemavu na wabunge huru,” inasema barua hiyo.

Wabunge hao wanaeleza kuwa kutengwa kwa viti maalum kutamsaidia Spika kuwatambua kwa urahisi wanapokuwa ndani ya ukumbi wa Bunge.

Aidha, wanataka uwakilishi maalum katika Kamati ya Uteuzi, ambayo husimamia kuweka wabunge katika kamati mbalimbali za Bunge, ili kulinda maslahi yao.
“Hili litahakikisha kundi la wabunge huru linatambuliwa rasmi badala ya kujumuishwa kwa jumla kama ilivyo sasa,” inasema barua hiyo.
Kwa mujibu wao, kwa sasa wanategemea hisani ya viongozi wa walio wengi na walio wachache katika ugavi wa nafasi za kamati.

“Tunapoenda kwa viongozi wa walio wengi na walio wachache, tunaambiwa hawawajibikii wabunge huru ambao hawajaegemea upande wowote. Matokeo yake ni kwamba wabunge huru huachwa nje ya kamati; kwa kweli wanabaguliwa na kupuuzwa kabisa,” inasema barua hiyo.

Wabunge hao pia wanataka sauti kubwa zaidi katika uundaji wa Kamati ya Hesabu za Umma (PAC), wakitaka kiti maalum kitengwe kwa mwakilishi wao.

Kwa sasa, Kanuni ya Kudumu 205(4) inaeleza kwamba katika uanachama wa PAC, vyama visivyo sehemu ya serikali ya kitaifa vinapaswa kuwa na wingi wa mwanachama mmoja.

Barua hiyo imeungwa mkono na wabunge wote 12 huru walio katika Bunge la Taifa. Hao ni Shakeel Shabbir, Caroline Ng’elechei (Elgeyo Marakwet), Monicah Marubu (Lamu), Joshua Mbithi (Masinga), Benard Muriuki (Mbeere Kusini), Elijah Njoroge (Gatundu Kaskazini), Ronald Karauri (Kasarani), Timothy Toroitich (Marakwet Magharibi), Fatuma Mohammed (Migori), Geoffrey Mulanya (Nambale), Kitilai Ole Ntutu (Narok Kusini) na Rahim Dawood (North Imenti).

Mbunge huru ni yule anayechaguliwa bila ufadhili wa chama chochote cha kisiasa. Kisheria, mtu anayepania kugombea kama mgombea huru lazima awe amejiuzulu kutoka chama chochote cha kisiasa angalau miezi mitatu kabla ya uchaguzi.

Hata hivyo, ingawa kisheria hawapaswi kuhusishwa na vyama vya kisiasa, wengi wa wabunge huru wanaochaguliwa hujiunga au kushirikiana na vyama au miungano ya kisiasa. Mara nyingi hufanya hivyo ili kupata nafasi katika kamati muhimu za Bunge na pia kusaidia serikali kupata idadi inayohitajika ya kura wakati wa maamuzi muhimu.

Katika siku za hivi majuzi pia kumekuwa na wito wa kuwafadhili wagombea huru kupitia Hazina ya Vyama vya Kisiasa, sawa na vyama vya kisiasa.

Mwaka jana, wakati wa mjadala kuhusu Mswada wa Marekebisho ya Sheria ya Vyama vya Kisiasa wa 2024, baadhi ya wabunge walipendekeza sheria ibadilishwe ili wagombea huru wanufaike na hazina hiyo.

Mbunge wa Suba Kusini, Caroli Omondi, alipendekeza wagombea huru wanaopata angalau asilimia tano ya kura zote zilizopigwa wanufaike na fedha hizo. Alisema Katiba inaruhusu mtu kuingia katika uongozi wa kisiasa kupitia chama cha kisiasa au kama mgombea huru, na kwamba hakuna njia iliyo bora kuliko nyingine.