Mke wa Besigye aomba kesi inayomwandama mumewe iahirishwe hadi apate nafuu
MKE wa kiongozi wa upinzani nchini Uganda, Kizza Besigye, Winnie Byanyima, amelaani kuendelea kwa kesi ya mumewe huku mwanasiasa huyo akiwa amelazwa kutokana na hali yake mbaya ya afya.
Besigye, 70, anakabiliwa na mashtaka ya uhaini yanayohusiana na madai ya kupanga njama ya kumpindua Rais Yoweri Museveni, ambaye amekuwa madarakani tangu 1986.
Byanyima, ambaye ni mkurugenzi mtendaji wa UNAIDS, amesema si haki kesi hiyo kuendelea wakati mumewe hawezi kufika mahakamani kwa sababu ya ugonjwa.
Amesema Besigye hawezi hata kuzungumza kutokana na hali yake.
Awali, mwanasiasa huyo alilazwa katika chumba cha wagonjwa mahututi baada ya kuanguka akiwa mahakamani, lakini alirejeshwa gerezani mapema mwezi huu licha ya madaktari kuonya kuhusu hali yake.
Besigye alikamatwa nchini Kenya mwaka 2024 na kupelekwa Uganda, ambako awali alifikishwa katika mahakama ya kijeshi kabla kesi yake kuhamishiwa mahakama ya kiraia.
Byanyima ameitaka serikali kumwachilia kwa dhamana ili apate matibabu yanayohitajika.