Habari

Azma ya Raila Jnr Kibra yachemsha Orero, Imran

Na CECIL ODONGO August 30th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

KUJITOSA kwa Raila Junior katika kinyang’anyiro cha ubunge wa Kibra, Nairobi, kumeanza kuzua pingamizi miongoni mwa baadhi ya wawaniaji wa ODM, huku mwana huyo wa aliyekuwa Waziri Mkuu Raila Odinga akisaka kiti hicho 2027.
Kibra kwa miongo imekuwa ngome ya kisiasa ya familia ya Odinga. Marehemu Raila aliwakilisha eneo hilo bungeni kuanzia 1992 hadi 2013, wakati Kibra ilikuwa sehemu ya Lang’ata.
Kila mara nchi ilipokabiliwa na maamuzi magumu ya kisiasa, Raila alirejea Kibra kutoa mwelekeo ambao baadaye ulikumbatiwa na maeneo mengine nchini.
Mnamo Novemba 30, 2009 wakati wa mvutano kuhusu uamuzi wa kufurusha watu kutoka msitu wa Mau, Raila alitangaza hadharani kwamba alikuwa tayari kurejea Kibra akapike mandazi iwapo suala hilo lingemgharimu kisiasa.
Kuingia kwa Raila Junior katika kivumbi hicho kumezua ushindani mkali wa kisiasa kati yake, mbunge wa sasa wa Kibra Peter Orero na aliyekuwa mbunge wa hapo Imran Okoth.
Junior amekuwa akishiriki miradi ya kijamii na kukutana na makundi mbalimbali huku akiweka misingi ya kampeni zake kuelekea 2027.
“Kibra ilikuwa ngome ya kisiasa ya babangu, na kama familia tumekuwa na safari ndefu pamoja na watu wa eneo hili. Nikichaguliwa nitamakinikia sana elimu kwa kuhakikisha basari zinapatikana ili pasiwe na mtoto anayekosa fursa ya kupata elimu,” mwana huyo mdogo wa Raila alisema katika mahojiano na Jamvi.
 “Najua baadhi ya sekta kama afya na maji zimekabidhiwa serikali za kaunti, lakini nitafanya kila niwezalo kuhakikisha huduma hizo zinafikia watu wa Kibra. Tutazingatia sana kuboresha maisha ya wakazi kwa kila njia iwezekanavyo,” akaongeza.
Junior pia alifichua kuwa kwa miaka mingi alikuwa miongoni mwa wandani waliompangia babake mikakati ya kisiasa huko Kibra.
Wiki hii mama yake, Ida Odinga, alipokuwa akisherehekea siku yake ya kuzaliwa, alitangaza kwamba amempa Raila Junior baraka za kutimiza ndoto zake za kisiasa, ikiwemo azma yake ya kuwania ubunge wa Kibra.
“Nyinyi watu wa Kibra mmeamua na sina chaguo jingine. Namkabidhi mwanangu mikononi mwenu. Viongozi mlio hapa mtunze, mfundishe na mpe mwongozo. Wengi wenu mlianza siasa pamoja na Baba. Mwonyesheni njia,” akasema Mama Ida.
Alisisitiza kuwa siasa za Junior zinapaswa kuwa safi na zisizo na matusi wala vurugu, akisema Kibra ilikuwa msingi wa safari ya kisiasa ya familia ya Odinga.
“Washawishi watu kwa maneno yako na uwaambie kile unachoweza kuwafanyia,” akasema.
Hata hivyo, mbunge wa sasa Orero anadai Junior anasukumwa na baadhi ya wawakilishi wadi (MCAs) maalum ambao hawana ushawishi wa kisiasa Kibra. Alisisitiza yuko tayari kukutana na Junior kwenye debe.
“Baadhi ya wawakilishi wadi maalum wanaomsukuma wamepoteza uchaguzi mara nne, na wanalenga maslahi yao binafsi. Hata hivyo, kazi yangu Kibra iko wazi kwa kila mtu kuona. Sina mpinzani. Aje tushindane, nami nitamshinda,” akahoji Orero.
Alishangaa kwa nini Junior amejitosa kwenye kinyang’anyiro hicho ilhali dada yake, Winnie Odinga, aliwahi kukinyemelea kabla kujiondoa na kuelekeza nguvu zake katika kivumbi cha useneta Nairobi.
Orero alisema licha ya kuwa karibu na familia ya Odinga hajazungumza na Mama Ida kuhusu azma ya Junior.
“Kuna nini cha kuzungumza? Junior ana haki yake ya kidemokrasia na sitaki kuwadharau au kuonekana niko kwenye vita nao. Waache watu waamue,” akasema mbunge huyo.
Kwa upande wake aliyekuwa mbunge Imran Okoth ametishia kuondoka ODM na kuwania kiti hicho kama mgombea huru iwapo chama hakitaendesha uteuzi wa haki na huru.
“Junior yuko huru kuja kuwania lakini ajue sisi ni wanachama wa ODM na tunasisitiza kusiwe na mapendeleo yoyote. Orero, Junior na mimi tushindane kwa haki, na atakayeshinda apewe tiketi ya ODM,” akahoji.