Habari

Azma ya Raila Jnr Kibra yachemsha Orero, Imran

Na CECIL ODONGO August 30th, 2026 Kusoma ni dakika: 3

KUJITOSA kwa Raila Junior katika kinyang’anyiro cha ubunge wa Kibra, Nairobi, kumeanza kuzua pingamizi miongoni mwa baadhi ya wawaniaji wa ODM, huku mwana huyo mdogo wa aliyekuwa Waziri Mkuu Raila Odinga akisaka kiti hicho 2027.
Kibra kwa miongo imekuwa ngome ya kisiasa ya familia ya Odinga. Marehemu Raila aliwakilisha eneo hilo bungeni kuanzia 1992 hadi 2013, wakati Kibra ilikuwa sehemu ya Lang’ata.
Kila mara nchi ilipokabiliwa na maamuzi magumu ya kisiasa, Raila alirejea Kibra kutoa mwelekeo ambao baadaye ulikumbatiwa na maeneo mengine nchini.
Mnamo Novemba 30, 2009 wakati wa mvutano kuhusu uamuzi wa kufurusha watu kutoka msitu wa Mau, Raila alitangaza hadharani kwamba alikuwa tayari kurejea Kibra akapike mandazi iwapo suala hilo lingemgharimu kisiasa.
Kuingia kwa Raila Junior katika kivumbi hicho kumezua ushindani mkali wa kisiasa kati yake, mbunge wa sasa wa Kibra Peter Orero na aliyekuwa mbunge wa hapo Imran Okoth.
Junior amekuwa akishiriki miradi ya kijamii na kukutana na makundi mbalimbali huku akiweka misingi ya kampeni zake kuelekea 2027.
 “Kibra ilikuwa ngome ya kisiasa ya babangu, na kama familia tumekuwa na safari ndefu pamoja na watu wa eneo hili. Nikichaguliwa, nitamakinikia sana elimu kwa kuhakikisha kuwa basari zinapatikana ili hakuna mtoto anayekosa fursa ya kupata elimu,” Raila Junior alisema katika mahojiano na Taifa Leo.
“Najua baadhi ya sekta, kama afya na maji, zimekabidhiwa serikali za kaunti, lakini nitafanya kila niwezalo kuhakikisha huduma hizi zinawafikia watu wa Kibra. Tutazingatia sana kuboresha maisha ya wakazi wa eneo hili kwa kila njia iwezekanavyo,” akaongeza.
Junior pia alifichua kwamba kwa miaka mingi alikuwa mmoja wa waliompangia babake mikakati ya kisiasa Kibra.
Wiki hii, mama yake, Ida Odinga, alipokuwa akisherehekea siku yake ya kuzaliwa, alitangaza kwamba amempa Raila Junior baraka za kutimiza ndoto zake za kisiasa, ikiwemo azma yake ya kuwania ubunge wa Kibra.
“Nyinyi watu wa Kibra mmeamua, na sina chaguo jingine. Namkabidhi mwanangu mikononi mwenu. Viongozi mlio hapa, mtunze, mfundishe na mpe mwongozo. Wengi wenu mlianza siasa pamoja na Baba. Mwonyesheni njia,” akasema Mama Ida.
Alisisitiza kwamba siasa za Junior zinapaswa kuwa safi na zisizo na matusi wala vurugu, akisema Kibra, ilikuwa msingi wa safari ya kisiasa ya familia ya Odinga.
“Washawishi watu kwa maneno yako na uwaambie kile unachoweza kuwafanyia,” akasema.
Hata hivyo, Bw Orero anadai kwamba Junior anasukumwa na baadhi ya wawakilishi wa wadi wateule ambao hawana ushawishi wa kisiasa Kibra. Alisisitiza kuwa yuko tayari kukutana naye kwenye uchaguzi.
 “Baadhi ya wawakilishi wadi maalum wanaomsukuma wamepoteza uchaguzi mara nne na wanalenga maslahi yao binafsi. Hata hivyo, kazi yangu kwa watu wa Kibra iko wazi kwa kila mtu kuiona. Kwa sasa sina mpinzani. Aje tushindane, nami nitamshinda,” akasema Bw Orero.
Mbunge huyo alishangaa kwa nini Raila Junior ameingia kwenye kinyang’anyiro hicho ilhali dada yake, Winnie Odinga, aliwahi kukinyemelea kabla ya kujiondoa na kuelekeza nguvu zake katika kinyang’anyiro cha useneta wa Nairobi.
 “Winnie alikuja kwangu mwenyewe na kuniambia kwamba anataka kuwania useneta wa Nairobi na kwamba hana nia tena ya kugombea Kibra. Sasa Raila Junior anasukumwa, lakini niko tayari. Ninaiheshimu familia ya Odinga na nina imani nitashinda uteuzi wa ODM,” akaongeza.
Bw Orero alisema licha ya kuwa karibu na familia ya Odinga, hajazungumza na Mama Ida kuhusu azma ya Junior.
“Kuna nini cha kuzungumza? Junior ana haki yake ya kidemokrasia na sitaki kuwadharau au kuonekana niko kwenye vita nao. Waache watu waamue,” akasema.
Bw Orero alisema wakati wa uongozi wake ameboresha elimu kuimarisha michezo pamoja na kujenga na kukarabati barabara kadhaa Kibra.
“Nilichofanya kinazidi kazi ya watangulizi wangu tangu 2013. Nimesambaza zaidi ya Sh65 milioni za bursari na, mbali na CDF, kuna miradi mingi tumekamilisha kupitia Benki ya Dunia. Mimi ni mbunge mwenye bidii, kwa hivyo atanishinda aje ?” akauliza.
Kwa upande wake, aliyekuwa mbunge Imran Okoth ametishia kuondoka ODM na kuwania kiti hicho kama mgombea huru iwapo chama hakitaendesha uteuzi wa haki na huru.
“Uteuzi wa 2022 haukuwa wa haki na huru. Mara hii, watu wanastahili kupata nafasi ya kumchagua kiongozi wanayemtaka badala ya kulazimishiwa mtu. Nimekuwa nikifanya kampeni na ninaamini mimi ndiye mtu anayefaa kuwa mbunge,” akasema Imran.
 Bw Imran alichukua kiti hicho kutoka kwa marehemu kaka yake, Ken Okoth kupitia uchaguzi mdogo mnamo 2019 na anasema miaka yake miwili madarakani iliacha rekodi inayoonekana ya maendeleo.
“Mbunge wa sasa hajafanya chochote, na Kibra inaanza kurejea ilivyokuwa awali. Nataka kurejea na kuendeleza kazi niliyoianza.
 “Junior yuko huru kuja kuwania, lakini anapaswa pia kujua kwamba sisi ni wanachama wa ODM na tunasisitiza kusiwe na mapendeleo yoyote. Orero, Junior na mimi tushindane kwa haki, na atakayeshinda apewe tiketi ya ODM,” akaongeza.