Viongozi wa Kenya Kwanza wazidi kuunga mkono Mung’aro achaguliwe tutam
GAVANA wa Kilifi, Bw Gideon Mung’aro, amezidi kuungwa mkono na viongozi wa Kenya Kwanza kutetea kiti hicho katika Uchaguzi wa 2027.
Spika wa Seneti, Bw Amason Kingi, alisema wanachama wa UDA Kilifi watamuunga mkono mgombea wa ODM.
Hii ni licha ya kuwa, spika wa zamani wa Bunge la Kaunti ya Kilifi, Bw Jimmy Kahindi, alichapishwa kunuia kuwania ugavana kwa tikiti ya UDA miezi sita iliyopita.
Akizungumza katika mkutano wa kisiasa Kilifi, Bw Kingi aliwataka wanachama wa UDA kutohisi wametelekezwa na uamuzi wa chama hicho kutowasilisha mgombea wa ugavana.
Bw Kingi pia aliwataka wanachama wa UDA kutomuunga mkono mgombea wa ugavana ambaye atakuwa mpinzani wa Bw Mung’aro, akisema hatua hiyo itakuwa kinyume na makubaliano ya kisiasa kati ya vyama hivyo.
Hata hivyo, Bw Mung’aro alisema yuko tayari kukabiliana na mgombea yeyote katika uchaguzi huo, akisema pia yuko tayari kushiriki mchujo wa ODM ili kupata tiketi ya chama hicho.
Msimamo wa Bw Kingi unatofautiana na ule wa Katibu Mkuu wa UDA, Bw Hassan Omar, ambaye amekuwa akipinga mpango wowote wa kugawana maeneo ya kisiasa kati ya UDA na ODM.