Dimba

Home Boys ndio mabingwa ligi ya ‘Weka Panga chini’

Na KALUME KAZUNGU August 26th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

KLABU ya Home Boys FC kutoka mtaa wa Gadeni ndiyo iliyotawazwa bingwa wa michuano ya ligi ya ‘Weka Panga Chini’ kisiwani Lamu.

Hii ni baada ya kuilaza timu ya Real Madrid kutoka mtaa wa Wiyoni magoli 2-1 kwenye fainali kali iliyochezewa katika uwanja wa Twaifu mjini Lamu Jumapili.

Ligi hiyo maalum ya mpira wa miguu ilishirikisha klabu 16 za Lamu za vijana wa chini ya miaka 18.

Ilizinduliwa mapema Agosti, dhamira kuu ikiwa ni kukabiliana na uhalifu wa mapanga na dawa za kulevya miongoni mwa vijana eneo hilo.

Wafadhili wakuu ni Idara ya Usalama kupitia kitengo cha Polisi wa Watalii (TPU), Bodi ya Utalii ya Lamu (LTA), Shirikisho la Kandanda Nchini (FKF) na serikali ya kaunti ya Lamu.

Fainali ilishuhudia idadi kubwa ya mashabiki waliofika kushangilia timu zao.

Mshindi wa kwanza (Home Boys FC) alituzwa Sh30,000 pesa taslimu, kikombe na jezi ilhali wa pili (Real Madrid FC) ikituzwa Sh20,000 na jezi.

Nambari tatu iliendea klabu ya Lamu Boys FC kutoka mtaa wa Langoni kisiwani Lamu, hivyo kupokea kitita cha Sh10,000 na jezi.

Mechi ya fainali ilihudhuriwa na kamanda wa polisi wa watalii (TPU) ukanda wa Pwani, Bw David Kabiru, aliyekariri wito wa vijana wa Lamu, Pwani na Kenya kwa jumla kuhubiri amani, kujiepusha na makundi ya uhalifu na dawa za kulevya.

“Nimefurahia kushuhudia soka tamu hapa kisiwani Lamu. Mfahamu kwamba mshindi si klabu ya Home Boys pekee eti kwa sababu imeshinda fainali. Wote walioshiriki ligi hii ni washindi. Ninaambiwa karibu vijana 270 wameshirikishwa kwenye michuano hii. Nyote mjue ni washindi na tuendelee kushirikiana kudumisha Amani,” akasema Bw Kabiru.

Mwenyekiti wa LTA, Bi Fridah Njeri aliahidi ushirikiano wake na wadau wengine ili kuona kwamba ligi nyingine sawia inaanzishwa kufikia Disemba mwaka huu.

“Tutahakikisha kila msimu wa likizo tunazindua ligi maalum ya soka ili tuwashughulishe vijana wetu na kuwaepusha na majanga, hasa mihadarati,” akasema Bi Njeri.

Naibu wa LTA, Bw Jamil Mbarak ambaye pia alihudhuria fainali ya ligi hiyo uwanjani Twaifu aliwashauri vijana kujiepusha na mizozo na hasira.

“Hasira hazijawahi kusuluhisha mambo. Tujifunze kudhibiti hasira zetu. Tujiepusha na mizozo na badala yake tupendane na kuhubiri amani ili Lamu iendelee kuwa kivutio bora cha watalii,” akasema Bw Mbarak.

Katibu wa kamati andalizi, ambaye pia ni Mwakilishi wa Vijana katika FKF, Lamu, Bw Athman Farid, maarufu Pirezi, aliwapongeza wanasoka wote walioshiriki ligi hiyo kwa kudumisha nidhamu kipindi chote cha wiki tatu ambapo ligi imekuwa ikiendelea.

Kwenye ligi hiyo, kiungo Mohamed Ali kutoka klabu ya Lamu Boys FC ndiye aliyetawazwa mfungaji bora akiwa na magoli 7 ilhali kipa bora akawa ni Mohamed Farid kutoka Real Madrid FC.

Mchezaji aliyeibuka bora na mwenye nidhamu zaidi ni Abdallah Abdulmalik kutoka Real Madrid FC ilhali mchezaji aliyetawazwa kuwa mwenye kipaji cha kutegemewa ni Daniel Chome kutoka timu ya Dragon Junior FC.

Wote walituzwa pesa taslimu na vyeti vya kutambua juhudi zao.