Habari

Mgomo JKIA wazua hasara, safari zikichelewa

Na DANIEL OGETTA August 31st, 2026 Kusoma ni dakika: 2

ABIRIAkatika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Jomo Kenyatta (JKIA) waliingiwa na wasiwasi na sintofahamu kuhusu safari zao baada ya wafanyakazi wa sekta ya anga kuanza tena mgomo.
Hali hiyo ilisababisha safari kadhaa za ndege ndani na nje ya nchi kucheleweshwa.
Wasafiri walisema hawakupewa taarifa ya kutosha kuhusu mgomo huo, huku baadhi yao wakifika uwanjani na kugundua kuwa safari zao zilikuwa zimecheleweshwa.
Muungano wa Wafanyakazi wa Usafiri wa Anga nchini (KAWU) ulianza tena mgomo Jumamosi usiku kutokana na malalamishi mbalimbali, yakiwemo yale yaliyosababisha kusimamishwa kwa mgomo wa awali mwezi uliopita.
Mwenyekiti wa KAWU Walter Ongeri aliambia Taifa Leo kuwa wafanyakazi waliamua kurejea kwenye mgomo baada ya serikali kushindwa kutekeleza masharti ya mkataba wa maelewano (MoU) uliotiwa saini na muungano huo.
“Tulitia saini makubaliano ya kurejea kazini lakini, kwa bahati mbaya, KAA na KCAA zimeshindwa kushughulikia malalamishi yetu. Asasi hizo mbili hazijajitolea kikamilifu katika mazungumzo na zimeshindwa kushirikiana nasi katika kutafuta suluhu ya malalamishi yetu,” akasema Katibu Mkuu wa KAWU Moss Ndiema.
 Glen Omindu, aliyekuwa anatarajia kusafiri Dubai kwa ndege ya saa saba mchana, alisema abiria hawakuwa wameambiwa wangetoka saa ngapi.
“Hakukuwa na onyo lolote na hilo ndilo tatizo. Ndege ilikuwa iondoke saa saba lakini bado hatujaambiwa tutasafiri lini. Tutalazimika kutafuta cha kufanya kwa sasa na ninatumai mambo yatakuwa sawa au niahirishe safari,” akasema Bw Omindu.
Faith Mbugua, aliyefika uwanjani saa nne asubuhi kwa safari yake ya saa saba, alisema abiria walikuwa wakihangaika kupata taarifa kuhusu safari yao.
“Tumechanganyikiwa sana. Tulikuwa hapa saa nne na tukaambiwa kuna mgomo. Safari yetu sasa imepangwa kuondoka saa 2:50 usiku,” akasema.
Stephen Maguro, aliyekuwa akisafiri Rwanda kuhudhuria mkutano, pia alisema safari yake ilikuwa imecheleweshwa.
Mamlaka ya Viwanja vya Ndege nchini (KAA) ilisema viwanja vya ndege kote nchini vilikuwa vikikumbwa na abiria kucheleweshewa safari.
“KAA inashirikiana kwa karibu na mashirika husika ya anga, kampuni za ndege na wadau wengine kudhibiti hali hiyo, kupunguza usumbufu na kuhakikisha shughuli za viwanja vya ndege zinaendelea kwa utaratibu,” akasema.
 KAA iliwashauri abiria kuwasiliana na kampuni zao za ndege kupata taarifa kuhusu safari zao.
Wakati huo huo, maafisa wa KAWU, Wizara ya Uchukuzi na mashirika ya anga walikuwa katika kikao cha dharura Jumapili kutafuta suluhu kuhusu mgomo.