Habari

Nimepunguza kasi ya madeni, asema Ruto

Na JUSTUS OCHIENG’ August 30th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

RAIS William Ruto ametetea vikali rekodi ya serikali yake kuhusu deni la taifa, akisema Kenya imefanikiwa kupunguza kasi ya kukopa ikilinganishwa na tawala mbili zilizotangulia.

Kwa mujibu wa Rais, kipimo muhimu si iwapo nchi imeacha kukopa kabisa, bali ni kiwango ambacho deni la umma limekuwa likiongezeka.

Alisema deni la taifa lilikuwa takriban Sh10.3 trilioni alipoingia madarakani mnamo 2022 na linatarajiwa kufikia karibu Sh13 trilioni kufikia mwisho wa mwaka huu, ongezeko analodai ni la asilimia 27 pekee katika kipindi cha miaka mitano.

“Moi alipoondoka madarakani, deni la taifa lilikuwa Sh630 bilioni. Kibaki alilirithi na kuliongeza hadi Sh1.8 trilioni ndani ya miaka 10. Hilo ni ongezeko la karibu mara tatu,” alisema Rais Ruto.

Aliongeza kuwa Rais Uhuru Kenyatta alipomaliza muhula wake 2022 aliacha deni la Sh10.3 trilioni, kiwango ambacho kilikuwa kimeongezeka mara tano kutoka alichokuta Kibaki.

“Katika miaka yangu mitano, deni limeongezeka kutoka Sh10.3 trilioni hadi Sh13 trilioni. Hilo si ongezeko la mara kadhaa bali ni asilimia 27 pekee,” alisema.

Kauli hiyo ndiyo msingi wa hoja yake kwamba, alitimiza moja ya ahadi zake kuu za kampeni za mwaka 2022 za kudhibiti tabia ya kukopa kupita kiasi.

“Nilisema ukiwa ndani ya shimo, jambo la kwanza ni kuacha kuchimba. Hivyo ndivyo tulivyokuta nchi ikiwa,” alisema.

Rais alisema alinuia kupunguza kutegemea mikopo, ushuru na madeni kwa kubadilisha jinsi miradi ya maendeleo inavyofadhiliwa.

Anasema serikali yake imeendelea kuwekeza katika miundombinu na miradi ya kijamii bila kuongeza deni la kawaida la serikali kwa kasi iliyoshuhudiwa miaka ya nyuma.

Miongoni mwa miradi mikubwa aliyotaja ni barabara ya Rironi-Nakuru-Mau Summit, Mradi wa Northern Kenya Gateway, upanuzi wa reli ya kisasa (SGR) kuelekea Kisumu na Malaba, pamoja na miradi ya maji na nishati.

Pia alitaja Mpango wa Nyumba Nafuu, ambao una zaidi ya nyumba 300,000 katika hatua tofauti za ujenzi, mabweni ya wanafunzi na masoko ya kisasa.

Kwa mujibu wa Rais, uwekezaji katika nyumba, masoko na mabweni pekee umefikia takriban Sh1.2 trilioni.

Hata hivyo, wakosoaji wake wanaonya kuwa kuangalia tu kiwango rasmi cha deni hakutoshi.

Wanasema kuna majukumu mengine ya kifedha yanayoibuliwa kupitia mbinu mbadala za ufadhili ambayo huenda hayajaonekana moja kwa moja katika deni rasmi la taifa.

Mojawapo ya hoja hizo ni kutumia mapato ya baadaye ya ushuru wa matengenezo ya barabara kama dhamana ya kufadhili miradi au kulipa wakandarasi.

Shirika la Fedha la Kimataifa (IMF) pia limekuwa likihimiza kutambuliwa kwa aina mbalimbali za madeni na wajibu wa kifedha yanayotokana na ushirikiano kati ya sekta ya umma na binafsi.

Rais Ruto anasema suluhisho lake ni kuanzisha Hazina ya Kitaifa ya Miundombinu, inayolenga kuvutia uwekezaji kutoka kwa sekta binafsi, hazina ya pensheni na taasisi za maendeleo badala ya kutegemea mikopo ya serikali pekee.

Lakini mafanikio ya mpango huo yatategemea uwazi, usimamizi na uwezo wa miradi hiyo kuzalisha mapato bila kuwaachia walipakodi mzigo wa siri wa kifedha.