Habari za Kitaifa

Ruto alicheza walimu? Ahadi ya nyumba za bei nafuu yakosa kutimia mwaka mmoja sasa

Na LYNET IGADWAH September 1st, 2026 Kusoma ni dakika: 3

WALIMU wamelalamika kuwa ahadi ambazo walipewa na Rais William Ruto kwenye mkutano ulioandaliwa Ikulu ya Nairobi mwaka mmoja uliopita, bado hazijatimizwa.

Wakati wa mkutano huo uliowashirikisha zaidi ya walimu 10,000, uliofanyika Septemba 13, 2025, Rais alitoa ahadi kadhaa za kushughulikia changamoto zao lakini hadi sasa hakuna kilichotimizwa.

Miongoni mwa ahadi kuu ilikuwa serikali kutenga asilimia 20 ya nyumba za gharama nafuu kwa walimu na kuongeza mara mbili idadi ya walimu wanaopandishwa vyeo kila mwaka hadi 50,000.

Ongezeko hilo lingesaidia kukabiliana na tatizo la walimu kukwama katika daraja moja ya kazi.

Hata hivyo, ahadi hiyo haijatimizwa kwa kuwa Tume ya Kuwaajiri Walimu (TSC) imetangaza nafasi 34,000 za kuwapandisha vyeo.

Hii inamaanisha asilimia 68 pekee ya ahadi hiyo imetimizwa.

Katibu Mtendaji wa Chama cha Walimu Nchini (KNUT) tawi la Nairobi Mugwe Macharia, alisema nafasi zilizotangazwa na TSC ni chache kuliko zilizoahidiwa.

“Hatujaona ongezeko la mara mbili la nafasi za kupandishwa vyeo kutoka 25,000 za sasa kwa sababu TSC imetangaza nafasi 30,000 pekee, na kuacha pengo la 20,000,” akasema Bw Macharia.

Rais pia aliahidi kupunguza muda wa kutekelezwa kwa Mkataba wa Makubaliano (CBA) wa 2025–2029 kutoka miaka minne hadi miwili na kuwapandisha walimu wa masomo wa masomo spesheli daraja moja la kazi.

Aidha, Rais aliahidi kuwapa walimu wakufunzi 20,000 ajira ya kudumu na pensheni, pamoja na kuagiza mabadiliko ya Mwongozo wa Maendeleo ya Kitaaluma (CPG) unaotumiwa na TSC katika kuwapandisha walimu vyeo.

Katibu Mkuu wa Muungano wa Walimu Shule za Upili na Vyuo Anuwai (KUPPET), Akello Misori, jana alisema utekelezaji wa ahadi hizo unategemea asasi husika za serikali.

“Mkutano huo haukuhusu CBA, kwa hivyo hatukujadili masharti hayo na Rais. Ikiwa alitoa ahadi fulani, hizo ni ahadi za kisiasa, na tunazifuatilia kupitia taasisi husika,” akasema Bw Misori.

Kuhusu ahadi kupunguza muda wa utekelezaji wa CBA kutoka miaka minne hadi miwili Bw Misori amesema utekelezaji halisi ulipaswa kujadiliwa kati ya walimu na TSC.

“Jambo la muhimu sana kwa walimu ni suala linalohusiana na CBA, ambalo Rais, akiwa mshirika, alipaswa tu kulianzisha ikiwa ingewezekana. Lakini hilo lilikuwa kati yetu na TSC ili litekelezwe,” akasema.

Kuhusu mabadiliko ya CPG, ambayo yamekuwa yakilaumiwa kwa kusababisha walimu kukwama katika daraja moja la kazi, TSC imependekeza CPG mpya ya 2026 itakayowaruhusu walimu kufikia daraja la juu zaidi bila kuacha kufundisha.

TSC pia imependekeza njia mbili tofauti za maendeleo ya taaluma, moja kwa walimu wanaoendelea kufundisha madarasani na nyingine kwa wanaotaka kushikilia nyadhifa za uongozi na utawala.

Hata hivyo, mapendekezo hayo bado hayajaanza kutekelezwa.

Knut, Kuppet na Muungano wa Walimu wa Elimu Maalum (KUSNET) walitia saini makubaliano hayo na TSC Juni 18, 2026, na kuyawasilisha kwa Tume ya Kutathmini Mishahara na Marupurupu ya Watumishi wa Umma (SRC) ili yapitiwe, lakini hakuna hatua zaidi iliyochukuliwa.

Katika utekelezaji wa ahadi ya kuwapandisha walimu wa masomo spesheli daraja moja ambao umekwama, Katibu mkuu wa KUSNET, James Torome, alisema CPG ya 2018 ilitoa nafasi kwa walimu hao kupandishwa madaraja mawili.

Hata hivyo, ahadi hiyo haikutekelezwa ndiyo maana walimwomba Rais aingilie kati.

Kuhusu nyumba za gharama nafuu, Kuppet ilisema mazungumzo yanaendelea kuhusu jinsi walimu watakavyopata asilimia 20 ya nyumba hizo kupitia mpango wa Boma Yangu.

“Tumekuwa tukishirikiana na wizara na idara inayohusika. Tumekutana na Waziri wa Nyumba na tumeunda kamati ya kiufundi kubaini jinsi walimu watakavyopata nyumba hizo,” akasema Bw Misori.

Kuhusu matibabu, TSC iliwahamisha walimu kutoka mpango uliokuwa ukiendeshwa na Minet Kenya hadi Mamlaka ya Afya ya Kijamii (SHA) Disemba mwaka jana.

Mpango huo unajumuisha matibabu ya kulazwa na kutolazwa, huduma za uzazi, magonjwa sugu, meno, macho, gharama za mazishi na matibabu nje ya nchi.

Bw Misori alisema muungano huo unaendelea kushirikiana na SHA kuhusu masuala ya kiufundi ili kuhakikisha walimu wanaendelea kunufaika na mpango huo.

“Vituo vya uzazi tayari vimetambuliwa na walimu tayari wanaenda kupata matibabu nje ya nchi,” akasema.

Hata hivyo, KNUT ilisema bado kuna changamoto katika SHA, huku baadhi ya hospitali zikikataa kuwahudumia walimu chini ya mpango huo mpya.