Maziwa yaisha madukani bei ikipanda katika maeneo mengi nchini
WAKENYA wanakabiliwa na uhaba wa maziwa katika maeneo mbalimbali nchini huku uzalishaji ukipungua na bei kupanda.
Takwimu rasmi ya Shirika la Takwimu la Kenya (KNBS) inaonyesha kuwa maziwa yaliyochukuliwa na kuuzwa katika nusu ya kwanza ya 2026 yalipungua kwa asilimia 0.6 hadi lita milioni 513.32 kutoka milioni 516.34 katika kipindi kama hicho mwaka uliopita.
Uhaba huo unashuhudiwa Nairobi, Nyeri, Kirinyaga, Embu, Mombasa, Homa Bay, Kisii na maeneo ya Nyanza na Magharibi.
Hata hivyo, Kisumu bado ina maziwa ya kutosha katika maduka makubwa, ingawa baadhi ya maduka madogo yaliripoti uhaba na bei ya juu.
Jijini Nairobi, nembo ya baadhi ya kampuni maarufu kama Brookside, Mt Kenya, New KCC na Tuzo zimekosekana katika sehemu ya kuuza maziwa kwenye maduka ya Naivas Moi Avenue.
Mtaani Donholm, mteja mmoja alisema bei ya pakiti ya maziwa ilipanda hadi Sh75 kutoka Sh60, huku wanunuzi wakiruhusiwa kununua pakiti tano pekee.
Willy Kimani, mwanzilishi wa Duka la maziwa la Jaza, alisema wasambazaji wamemweleza kuwa mabadiliko ya hali ya hewa yamesababisha upungufu wa maziwa.
“Kile ambacho wawasilishaji wa bidhaa wametuambia ni kwamba hali hii imetokana na mabadiliko ya hali ya hewa. Wameahidi kuwa hali itarejea kama kawaida mnamo Oktoba,” akasema Bw Kimani.
Katika kaunti za Nyeri, Kirinyaga na Embu, nusu lita imepanda hadi Sh48 kutoka Sh44 kutokana na uhaba wa malisho ya mifugo.
Wakulima wanaowasilisha maziwa kwa Kampuni ya Maziwa ya Mukurwe-ini, Nyeri wanasema uzalishaji umepungua kutoka lita 80,000 hadi 60,000.
Mombasa na maeneo ya Pwani, pakiti ya mililita 500 imefikia Sh75 kutoka Sh60.
Wafanyabiashara walisema mahitaji yameongezeka huku wasambazaji wakipunguza kiasi cha maziwa wanachopeleka madukani.
Kule Homa Bay, bei ya katoni yenye pakiti 12 za mililita 500 imepanda kutoka Sh620 hadi Sh750. Kisii pia imeripotiwa kukumbwa na uhaba huo huku wauzaji wakipokea kiwango cha chini cha maziwa.
– Ripoti za Kabui Mwangi, Gitonga Marete, George Munene, Winnie Atieno, George Odiwuor, Wycliffe Nyaberi na Domnic Ombok