Safari za ndege zakwama sababu ya mgomo baadhi ya wasafiri wakishauriwa kutumia treni
ABIRIA waliokuwa wakisafiri kuelekea Nairobi na Entebbe kupitia Uwanja wa Kimataifa wa Ndege wa Kisumu jana walikwama kwa muda mrefu huku shughuli uchukuzi angani zikitatizwa.
Mgomo wa Muungano wa Wafanyakazi wa Viwanja vya Ndege (KAWU) ambao unaingia siku yake ya tatu leo ndio ulisababishia abiria kadhia hiyo ya safari.
Miongoni mwa waliokwama ni Kaimu Katibu wa Kaunti ya Siaya, Elizabeth Adongo, ambaye safari yake ya Safarilink kuelekea Nairobi ilisukumwa mbele baada ya kukaa uwanjani kwa saa kadhaa.
Bi Adongo alisema alifika Uwanja wa Ndege wa Kisumu saa moja asubuhi ili asafiri hadi Nairobi, ambako alitarajiwa kuhudhuria mkutano muhimu wa kaunti saa nne asubuhi.
Hata hivyo, alisema alikaa uwanjani kwa saa kadhaa bila kupewa taarifa kuhusu hatima ya safari yake.
Bi Adongo alisema baadaye alipokea ujumbe kutoka kwa shirika hilo ukimfahamisha kuwa safari ilikuwa imeahirishwa.
“Ujumbe kutoka Safarilink ulifika karibu saa saba mchana ukisema safari ilikuwa imeahirishwa,” alisema.
Abiria mwingine, Lennox Omondi, mfanyakazi wa Serikali ya Kaunti ya Siaya, pia aliathiriwa na mgomo huo.
Baada ya kupokea ujumbe wa kuahirishwa kwa safari yake saa saba mchana, Bw Omondi alielekea kituo cha mabasi na akaamua kusafiri kupitia barabara.
Usumbufu huo uliwaacha abiria wengi uwanjani, huku baadhi wakitafuta njia mbadala za kufika walikokuwa wakielekea.
Kufikia Jumatatu alasiri, uongozi wa Uwanja wa Ndege wa Kisumu ulikuwa katika kikao cha dharura kutathmini hali na kupanga hatua za kuchukua.
Baadhi walibaki uwanjani wakisubiri taarifa kutoka kwa mashirika ya ndege na mamlaka ya nyuga za ndege, huku wengine wakiachana na mipango ya kusafiri kwa ndege na kutumia mabasi.