Habari za Kaunti

Wavinya akataa marekebisho ya madiwani kupunguza bajeti ya kaunti

Na PIUS MAUNDU September 2nd, 2026 Kusoma ni dakika: 2

MZOZO wa bajeti kati ya Gavana wa Machakos Wavinya Ndeti na baadhi ya madiwani wa Bunge la Kaunti umechacha baada ya gavana huyo kukataa marekebisho yaliyofanywa kwenye bajeti ya Sh17.8 bilioni ya mwaka wa kifedha wa 2026/2027.

Hatua hiyo imeibua makabiliano mapya katika Bunge la Kaunti, huku madiwani wakiwa na chini ya wiki mbili za kutathmini upya uamuzi wa kupunguza Sh853 milioni kutoka kwa bajeti hiyo.

Bi Ndeti aliwasilisha barua ya kupinga marekebisho hayo alipofika katika Bunge la Kaunti Jumatatu akiwa ameandamana na Katibu wa Kaunti Muya Ndambuki, Waziri wa Fedha Catherine Mutanu na maafisa wengine wakuu.

Alimkabili Karani wa Bunge la Kaunti Peter Mbatha, akimshtumu kwa kushirikiana na Spika Anne Kiusya kumzuia kuwasilisha mapendekezo yake.

“Kwa nini usipokee tu barua hiyo kama sheria inavyohitaji na uniachie nikabiliane na madiwani?” akamuuliza Bw Mbatha.

Baada ya barua hizo kupokewa, Bi Ndeti alisema hawezi kuidhinisha bajeti iliyorekebishwa kwa sababu inatishia huduma muhimu kwa wakazi.

“Siwezi kutia saini bajeti inayokiuka wazi mipaka iliyowekwa kisheria, kubomoa huduma muhimu za umma na kuhatarisha moja kwa moja maisha ya watu wetu,” akasema.

Marekebisho hayo yameathiri zaidi fedha za miradi ya barabara na baadhi ya mipango muhimu ya gavana, ikiwemo Huduma ya Vijana ya Machakos, mpango wa maziwa kwa watoto wa shule za chekechea na mpango wa mikopo nafuu uliotengewa Sh100 milioni.

Bi Ndeti anasema kupunguzwa kwa fedha kutalemaza utoaji wa huduma, huku madiwani wanaomuunga mkono wakisisitiza kuwa walifanya marekebisho hayo baada ya kuchunguza matumizi yenye utata.

“Gavana anaita mabadiliko haya kupunguzwa kwa bajeti. Sisi tunaita uchunguzi wa bajeti, kuweka kipaumbele upya na kugawa fedha upya. Tunapinga ubadhirifu na kurudiwa kwa miradi. Tunataka thamani ya fedha,” akasema Diwani wa Kalama, Bw Boniface Maeke.

Mzozo huo unaendeleza mvutano wa kisiasa kati ya Bi Ndeti na baadhi ya madiwani.

Waziri wa Fedha, Bi Mutanu amekuwa katikati ya mzozo huo baada ya kufutwa kazi na gavana Julai, siku ambayo Bi Ndeti alikabiliwa na hoja ya kumtimua.

Bi Mutanu alirejeshwa kazini wiki moja baadaye baada ya Mahakama Kuu kuingilia kati.

Mzozo wa sasa ulianza baada ya Bunge la Kaunti kuruhusu gavana kutumia asilimia 50 ya bajeti ya 2026/2027 kusubiri kupitishwa kwa Mswada wa Matumizi.