Habari za Kaunti

Kambi afichua atazindua chama cha Pwani kujipa ushawishi kama DCP ya Gachagua Mlimani

Na WINNIE ATIENO September 1st, 2026 Kusoma ni dakika: 2

UFICHUZI wa aliyekuwa Waziri wa Leba, Bw Kazungu Kambi, kwamba anapanga kuzindua chama kipya cha kisiasa, umeibua mwelekeo mpya wa kisiasa katika eneo la Pwani kuelekea kwa Uchaguzi Mkuu wa Agosti 10, 2027.

Kulingana na Bw Kambi, Rais William Ruto alipokutana naye katika Ikulu ya Nairobi mnamo Julai alimuuliza iwapo alikuwa na chama, akamwambia kuna vyama vitatu ambavyo angechagua kimoja kwa ajili ya mpango wake wa kuwania ugavana Kilifi.

Picha za mkutano huo zilisababisha mdahalo mkali ziliposambazwa mitandaoni, hasa ikizingatiwa kuwa mbunge huyo wa zamani wa Kaloleni wiki chache awali alikuwa mmoja wa wajumbe wa Mijikenda waliokutana na kinara wa Chama cha Democray for the Citizens Party (DCP), Bw Rigathi Gachagua, katika Kaunti ya Kwale.

“Nilipoitwa na Rais Ruto hivi majuzi, tuliongea kuhusu siasa. Aliniuliza kama nina chama. Nilimwambia kuna vyama vitatu na nitachagua kimoja ambacho tutakizindua rasmi hivi karibuni. Ni chama cha wakenya, si cha Wamijikenda pekee,” alisema, kwenye mahojiano ya redio.

Bw Kambi alisema chama hicho kinalenga kuwaleta pamoja watu wote wanaoishi Pwani, na viongozi watakuwa kutoka jamii zote nchini.

“Mimi nataka umoja wa Pwani kwa sababu kwa sasa hatuna umoja. Tuna utajiri, lakini tatizo la umaskini Pwani si watu wa nje. Tatizo ni sisi wenyewe, Wapwani. Kitu cha kwanza, hatupendani; pili, tuna fitina,” alisema.

Hatua hiyo imetokea wakati ambapo vyama vingi vya kisiasa vilivyoanzishwa Pwani vimekosa nguvu.

Chama cha Pamoja African Alliance (PAA) ambacho kiliundwa kabla uchaguzi uliopita, kiliamua hakitasimamisha wagombeaji katika uchaguzi ujao na badala yake kitaunga mkono wagombeaji wa UDA.

Hatua hiyo imewaacha wanasiasa waliokitumia kuwania viti 2022 na waliotarajia kukitumia mwaka ujao katika njiapanda, huku wengine wakilazimika kutafuta vyama vipya.

Bw Kambi alisema aliporejea katika siasa alijaribu kufufua vyama vya Kadu-Asili na Shirikisho kwa kushirikiana na wamiliki wa awali, lakini juhudi hizo hazikufanikiwa, hali iliyowalazimu kuanzisha chama kipya.

Aliongeza kuwa, hatua ya PAA imeathiri mipango mingi ya siasa za Pwani.

“Sitaki kudandia chama cha mtu, nataka tuwe na chama chetu. Tulikuwa na Shirikisho ambacho kilianzishwa na aliyekuwa Waziri wa Uchukuzi Bw Chirau Makwere lakini kilinunuliwa,” alisema.

Alisema dhamira yake ni kusaidia wakazi wa Kilifi na kuimarisha umoja wa Pwani.

Bw Kambi pia alionya dhidi ya siasa za ukabila na ubaguzi, akisema jamii zote zinazoishi Pwani zinapaswa kuchukuliwa kuwa wenyeji.

Alimpongeza Bw Gachagua kwa kuanzisha chama chake na kutetea maslahi ya watu wa Mlima Kenya, akisema kila jamii ina haki ya kuwa na jukwaa la kisiasa la kuwasilisha maslahi yake.

“Ni Wapwani peke yao ambao wamekuwa na vyama lakini hawako pamoja,” alisema.