TSC yatangaza nafasi 1,631 kwa walimu wanaotaka kupanda ngazi
TUME ya kuajiri walimu (TSC) imetangaza upya nyadhifa 1,631 za kuwapandisha cheo wasimamizi wa shule, na kuwapa fursa nyingine walimu wanaomezea mate nyadhifa za uongozi huku kukiwa na uhaba wa wasimamizi waliothibitishwa katika shule za umma.
Nyadhifa hizo zinajumuisha nafasi 1,470 za Naibu Mwalimu mkuu, 132 Naibu Mwalimu Mkuu III na 29 za Mwalimu Mkuu II katika shule za msingi na sekondari.
Tume imealika maombi kutoka kwa walimu wanaohudumu waliofuzu kujaza nafasi hizi za kupandishwa cheo kuambatana na Mwongozo wa Maendeleo Kitaaluma kwa Walimu.
Maombi ni sharti yapokewe kufikia usiku wa manane Jumatatu Septemba 14, 2026, ilisema TSC katika notisi.
Tangazo hilo jipya limejiri wiki chache tu baada ya Tume kuzindua mchakato wa kupandisha cheo uliojumuisha walimu 34,016 katika daraja zote, katika kile kilichotajwa kuwa moja kati ya shughuli kubwa zaidi za maendeleo kitaaluma katika miaka ya majuzi.
Shughuli hiyo iliyotangazwa Julai, iliangazia nyadhifa kuanzia Mwalimu wa Ngazi ya Juu II hadi Mwalimu Mkuu na ilijumuisha nyadhifa za kufundisha, usimamizi wa shule, kuboresha mtaala na vyuo vya mafunzo ya walimu.
Nyadhifa mpya zilizotangazwa ni muhimu, kwa sababu zinalenga nafasi za usimamizi wa shule wakati ambapo maelfu ya shule za umma zinaendeshwa bila wasimamizi waliothibitishwa.
Mchakato huo wa kupandisha vyeo umejiri kukiwa na malalamishi kuhusu kukwama kitaaluma katika huduma ya kufundisha.
TSC ilieleza Bunge kwamba walimu 178,871 wa shule za msingi na sekondari wamesalia katika daraja lile lile la kazi kutokana na upungufu kwenye bajeti, huku tume ikisema inahitaji mabilioni kushughulikia suala hilo.
Tume ilisema sehemu kubwa ya walimu waliokwama kitaaluma ni kutoka gredi C3 kwa walimu wa sekondari na gredi C1 kwa walimu wa shule ya msingi ambapo waelimishaji wengi wamesalia kwa miaka mingi licha ya kutimiza viwango vya kufuzu kupandishwa cheo.
“Tunaitaka TSC kutangaza mara moja nyadhifa za kuwapandisha vyeo walimu 135,000 ambao wamekwama katika daraja zao za kazi,” alisema Katibu Mkuu wa Kuppet, Bw Akello Misori.