Hasira kuhusu kutekwa kwa mhariri wa Standand Group Alex Kiprotich
MASHIRIKA ya habari nchini yameitaka Serikali kufanya uchunguzi huru na wa haraka kuhusu madai ya kutekwa kwa Mhariri Mwandamizi wa Standard Group, Alex Kiprotich.
Wameonya kuwa mashambulizi dhidi ya wanahabari yanazua hofu nchini kuelekea uchaguzi mkuu wa 2027.
Bw Kiprotich alitekwa na wanaume waliokuwa na silaha katika barabara ya Gilgil-Nakuru Jumanne usiku, muda mfupi kabla ya saa tatu na dakika 20 usiku.
Video ya tukio hilo inaonyesha gari aina ya Subaru lenye nambari ya usajili KDC 125E likimpita kisha kumzuia.
Wanaume waliokuwa na silaha walimwamuru atoke kwenye gari lake kabla ya kumwingiza kwa lazima katika gari lao.
Alipatikana ametupwa karibu na Bwawa la Masinga, Machakos Jumatano asubuhi, zaidi ya saa tisa baada ya kutekwa; umbali wa zaidi ya kilomita 200 kutoka eneo la tukio.
Bw Kiprotich alipewa hifadhi na familia moja ya eneo hilo kabla ya kikosi cha Standard Group kilichoongozwa na Afisa Mkuu Mtendaji wa kampuni hiyo, Chaacha Mwita, kumchukua karibu saa kumi na mbili na nusu asubuhi.
Alikuwa salama kimwili lakini alishtuka sana kiasi cha kutoweza kuzungumza na wanahabari.
Tukio hilo limeibua hasira miongoni mwa mashirika ya habari na ya kutetea haki za binadamu, huku yakitaka waliohusika kutambuliwa na kufikishwa mahakamani.
Chama cha Wahariri Kenya, Chama cha Wanahabari Kenya (KUJ) na Chama cha Wanawake katika Habari Kenya (AMWIK), chini ya Kenya Media Sector Working Group, vilisema tukio hilo ni sehemu ya mfululizo wa vitisho dhidi ya wanahabari.
Katibu Mkuu wa KUJ, Eric Oduor, alisema shambulio dhidi ya mwanahabari yeyote ni shambulio dhidi ya uhuru wa vyombo vya habari.
Alisema uchunguzi wa awali umebaini baadhi ya watu waliohusika na tukio hilo na kwamba mashirika hayo yatawasilisha malalamishi kwa Mamlaka Huru ya Kusimamia Utendakazi wa Polisi (IPOA) na Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashtaka ya Umma (ODPP).
“Tutaandikia ODPP ichukue hatua na iwapo haitafanya hivyo, tutawafungulia mashtaka maafisa waliohusika,” alisema Bw Oduor.
Hofu zaidi imezuka kutokana na madai kwamba mwezi Juni 27 pia kulikuwa na jaribio jingine la kumteka Bw Kiprotich.
Uchunguzi wa ndani wa Standard Group kuhusu tukio hilo umedaiwa kubaini gari lililotumiwa na watekaji ni la kitengo cha Crime Research and Intelligence Bureau (CRIB) cha Polisi, lakini hakuna afisa aliyewajibishwa.
Rais wa Chama cha Wahariri Kenya, Zubeida Kananu, alisema kushindwa kuwachukulia hatua wahusika wa mashambulizi ya awali kumewapa ujasiri wanaowalenga wanahabari.
Viongozi hao pia walielezea wasiwasi kuhusu kushuka kwa Kenya katika orodha ya uhuru wa vyombo vya habari duniani ya Reporters Without Borders (RSF).
Kenya imeshuka kutoka nafasi ya 69 mwaka 2022 hadi ya 106 kati ya nchi 180.
Chama cha Wamiliki wa Vyombo vya Habari (MOA) pia kimetaka kufanywe uchunguzi huru, wa haraka na wa wazi.
Mwenyekiti wake Agnes Kalekye alisema chama hicho kimehuzunishwa na tukio hilo lakini kimefarijika kwamba Bw Kiprotich alipatikana akiwa hai.
Alisisitiza kuwa wanahabari wanapaswa kuruhusiwa kutekeleza majukumu yao bila vitisho au kuingiliwa.
Rebecca Mutiso, meneja wa Uhuru wa Vyombo vya Habari na Utetezi katika Baraza la Vyombo vya Habari Kenya, aliwataka watu walio na malalamishi kutumia njia halali za kuyatatua badala ya kuwalenga wanahabari.
“Leo unataka kumnyamazisha mwanahabari, lakini itakuwaje haki zako zitakapokiukwa na uhitaji mwanahabari huyo huyo kuripoti kisa chako?” akauliza.
Amnesty International Kenya pia imetaka uchunguzi huru na wa uwazi, ikisema tukio hilo ni tishio kubwa kwa uhuru wa kujieleza na vyombo vya habari.