Maoni

MAONI: Caroli Omondi ni mwanamikakati stadi ambaye hucheza chini ya maji

Na PAUL NABISWA September 2nd, 2026 Kusoma ni dakika: 2

MMOJA wa wanasiasa ambaye anategemewa kwa mustakabali wa umoja wa upinzani ni Mbunge wa Suba Kusini Caroli Omondi.

Zipo sababu kadhaa zinazomkweza Caroli katika siasa Kenya inapojiandaa katika uchaguzi mkuu ujao wa Agosti 10, 2027.

Kwanza, yeye ndiye msemaji wa kundi la Linda Mwananchi linaloongozwa na seneta wa Nairobi Edwin Sifuna na washirika wake.

Pili ni katibu mkuu wa muungano wa Azimio, vyama ambavyo viliunga mkono Raila Odinga katika uchaguzi mkuu wa Agosti 8, 2022.

Moja ya sifa kubwa ya Caroli ni kuwa msemaji bora wa lugha zote mbili ila Kingereza chake kinashuka taratibu na kwa ufundi mkubwa.

Inawezekana Linda Mwananchi ilimteua bila kufahamu usuli wake vizuri.

Caroli ana tajiriba kubwa ya upatanishi na alikuwa kiungo muhimu kwa upande wa aliyekuwa kiongozi wa ODM Raila wakati wa mazungumzo baada ya ghasia za uchaguzi za 2007/2008.

Katika mahojiano yangu awali kidogo, aliniambia zile wanazoita mitaani “za ndani” yaani habari ambazo ni siri.

Ila sasa Caroli ana jukumu kubwa mno kupita Edwin Sifuna, Babu Owino, James Orengo na kundi lile jingine la Kalonzo Musyoka.

Anatakiwa kuhakikisha makundi haya yanapatana na mgombea mmoja kukabiliana na Rais William Ruto ambaye anataka ridhaa nyingine ya Wakenya.

Awali nyufa zimeanza kujitokeza katika kundi la Linda Mwananchi kuhusu anayestahili kuwa kiongozi wa chama na hata mgombea Urais.

Pili, Kalonzo, Gachagua na washirika kila mtu anapaza sauti kuwa anatosha kuongoza Kenya.

Tatu anatoka eneo la Nyanza ambalo linadai kuwa Raila Odinga aliwaacha kwa serikali jumuishi.

Caroli alionyesha makali yake kwa kufanikisha ziara ya Linda Mwananchi katika kaunti ya Homa Bay.

Pamoja na kuwa kulikuwa na vurugu kubwa na kusababisha maafa, kikosi cha Caroli kilifanikiwa kuuza sera kwa wakazi wa Homa Bay licha ya kuwepo kwa vitisho kutoka kwa wafuasi wa Gavana Gladys Wanga ambaye ndiye mwenyekiti wa chama cha ODM.

Moja ya dhima muhimu inayomsubiri ni kufifisha nguvu za ODM ambazo wahafidhina kutoka eneo lake hawadhanii kuwa ni jambo linalowezekana kwa wepesi.

Ruto alipo anajua uwezo wa ungaunga za Caroli.

Upinzani nao una mtihani mkubwa kumpa dhamana ya kusimamia mchakato wa kuupatanisha na kusalia kama gundi endapo watataka kuwa wenyeji wa ikulu.

Wafuasi wa Sifuna wanamtaka debeni, Matiang’i anasema ataikomboa nchi, Kalonzo ana huu wakati pekee huku Gachagua akijigamba kuwa nyota yake inaangaza.

Kazi kwa Caroli. Je, ataonyesha njia ya upinzani ya 2002?

Paul Nabiswa ni mhariri, NTV