Anajuana na kina Sifuna? Kivutha abadili jina la chama, sasa kuwa ‘The Mwananchi Party’
ALIYEKUWA Gavana wa Makueni Kivutha Kibwana anataka kubadili jina la chama chake cha Muungano Party (MP) kuwa The Mwananchi Party (TMP), hatua ambayo imeibua maswali kuhusu uhusiano wake na vuguvugu la Linda Mwananchi linaloongozwa na Seneta wa Nairobi Edwin Sifuna.
Hatua hiyo pia inaweza kuwa sehemu ya mikakati ya Profesa Kibwana kujiandaa kisiasa kabla ya uchaguzi mkuu wa 2027.
Bw Sifuna na washirika wake katika Linda Mwananchi wamekumbwa na pigo kubwa kisiasa katika wiki za hivi majuzi baada ya Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Kisiasa (ORPP) kuzuia juhudi zao za kusajili rasmi jina hilo.
Huku wakikumbana na vikwazo katika juhudi za kulinda jina la vuguvugu hilo, Profesa Kibwana aliwasilisha stakabadhi za kuomba kubadili jina la chama chake.
Si siri kwamba Profesa Kibwana amekuwa akimuunga mkono Bw Sifuna na vuguvugu lake kupitia mitandao ya kijamii.
Katika tangazo la gazeti rasmi la serikali la Agosti 24, Msajili wa Vyama vya Kisiasa John Cox Lorionokou alisema Muungano Party imewasilisha ombi la kubadili jina.
“Kwa kutumia mamlaka niliyopewa chini ya kifungu cha 20(1)(d) cha Sheria ya Vyama vya Kisiasa, Msajili wa Vyama vya Kisiasa anatoa taarifa kwamba Muungano Party (MP) inakusudia kubadili jina na kuwa The Mwananchi Party (TMP),” ilisema taarifa hiyo.
Msajili aliwaalika watu walio na pingamizi kuwasilisha maoni yao kwa maandishi katika muda wa siku saba tangu kuchapishwa kwa tangazo hilo.
Hata hivyo, muda huo sasa umekamilika bila pingamizi zozote.
Profesa Kibwana hakujibu maswali kuhusu sababu ya kubadili jina la chama na iwapo ana mpango wa kushirikiana na wanasiasa wa Linda Mwananchi 2027.
Hivi majuzi Bw Lorionokou alisema kuwa Liberty National Democratic Alliance Party, almaarufu LINDA Party, pamoja na Mwananchi Party, zilikuwa katika mchakato wa kusajiliwa.
Alisema hali hiyo ndiyo iliyofanya Bw Sifuna na washirika wake kunyimwa jina la Linda Mwananchi baada ya kubainika kuwa majina hayo yalikuwa tayari yamehifadhiwa.
Kwa mujibu wa ORPP, LINDA Party ilihifadhi jina lake Novemba 15, 2024.
Msajili pia alisema ombi la kuhifadhi jina Mwananchi Party liliwasilishwa na Pius Onyango Julai 2026 na bado linazingatiwa.
Hii inamaanisha kuwa jina hilo haliwezi kuchukuliwa na kundi jingine bila mchakato huo kukamilika.