Ruto aagiza sheria ipitishwe kuzuia wageni kufanya uchuuzi Kenya
RAIS William Ruto amesema kwamba haikubaliki kwa raia wa kigeni kuja nchini kufanya uchuuzi na biashara ndogo ndogo.
Anasema wageni wana ruhusa ya kuwa wawekezaji pekee, sio kushindana na wenyeji katika biashara ndogo kama uchuuzi na maduka madogo madogo.
Akizungumza baada ya kukutana na sehemu ya wafanyabiashara waliofanya maandamano wiki jana kulalamikia ushuru mpya wa KRA kuhusu shehena ya bidhaa za kutoka nje katika Ikulu ya Nairobi Jumatano, Rais aliagiza mawaziri husika kuharakisha mswada bungeni unaoharamisha aina fulani ya biashara kufanywa na raia wa kigeni.
“Tuko na wafanyabiashara kutoka nchi zingine, wacha nisiseme nchi gani, wamekuja hapa na kuwa wachuuzi, wanauza duvets. Bw Mukwana na Lee Kinyanjui, tayari tuko na mswada bungeni kuhusu mambo ya biashara. Katika hiyo bill, tumesema kuna biashara mgeni hawezi kufanya hapa Kenya by law. Nataka mketi chini na hawa wafanyabiashara muangalie na tuzibe mianya yote. Isitokee kwamba mtu ametoka China na amekuja kuwa hawker au kuuza duka kidogo hapo. Ichungwa, you don’t need any further instructions. Monday muamkie hiyo biashara. Hao wachuuzi wote wanafanya hii biashara kidogo kidogo wafunge na wasipofunga (ashangiliwa) tutafunga. Hatujajenga Investor Confidence ndio watu wakuje kuwa wachuuzi. Tumejenga Investor Confidence ndio watu wakuje kuwekeza,” akasema Bw Ruto.
Katika maandamano ya Agosti 28, 2026, waandamanaji walikusanyika katika eneo la Archives kabla ya kuelekea makao makuu ya KRA katika jengo la Times Tower katikati mwa jiji.
Wafanyabiashara hao walisema mabadiliko ya kiwango kinachotumiwa kukadiria thamani ya bidhaa za uagizaji yameongeza gharama za biashara na kupunguza faida zao.
Kwa mujibu wao, KRA imepandisha kiwango cha ukadiriaji kutoka 2.5m hadi 3.2m, hatua wanayodai imeongeza kwa kiasi kikubwa kodi inayolipwa kwa bidhaa zinazoagizwa kutoka nje, hususan kutoka China.
Walisema mabadiliko hayo yamesababisha ongezeko la takriban asilimia 28, huku thamani ya bidhaa kwa madhumuni ya kodi ikiongezeka kutoka Sh2.5 milioni hadi Sh3.2 milioni.