Habari za Kitaifa

Moto wateketeza msitu wa Aberdare siku nne mfululizo

Na WAIKWA MAINA September 3rd, 2026 Kusoma ni dakika: 2

MOTO umeteketeza Msitu wa Aberdare siku nne mfululizo huku hifadhi wanyamapori, miti na maeneo muhimu ya vyanzo vya maji yakiteketea.

Moto huo unateketeza Msitu wa Ndaragwa, eneo la Shamata, sehemu muhimu ya vyanzo vya maji ya Ziwa Olbolosat, Ol Kalou na maeneo mengine ya Ndaragwa.

Maafisa wanashuku kuwa moto huo ulianzishwa kwa bahati mbaya na waliokuwa waliokuwa wakirina asali msituni.

Hata hivyo, baadhi ya wakazi wanasema kuna imani ya zamani kwamba kuchoma msitu wakati wa ukame husaidia kuvuta mvua.

Wanaamini moshi mweusi unaotokana na moto huunda mawingu ambayo baadaye huleta mvua.

Serikali ya Kaunti ya Nyandarua na Huduma ya Misitu Kenya (KFS), ambazo zinaongoza juhudi za kuzima moto huo, zimesema zimelemewa na zinahitaji msaada wa dharura kutoka kwa mashirika mengine ya kuhifadhi mazingira na serikali ya kitaifa.

Afisa Mkuu wa uhifadhi wa misitu wa Nyandarua Daniel Mkung alisema moto huo unateketeza eneo la nyanda za juu lenye mimea mikavu, hali inayofanya iwe vigumu kuuzima.

“Moto uko katika eneo la nyanda za juu ambako kuna mimea mingi mikavu. Hali hii inafanya iwe vigumu zaidi kuudhibiti. Tunahitaji msaada wote tunaoweza kupata na tunapanga jinsi ya kuwasafirisha wazima moto zaidi hadi msituni,” alisema.

Alisema uchunguzi wa awali unaonyesha kuwa wachunaji wa asali huenda ndio walianzisha moto huo.

Hata hivyo, imani kuhusu moshi kuvuta mvua imeibua mjadala mwingine kuhusu sababu ya moto za mara kwa mara msituni wakati wa ukame.

Jackson Kieru, mwenye umri wa miaka 86, alisema baadhi ya watu bado wanaamini moshi wa moto huvuta mvua.

“Baadhi ya watu wanaamini moshi mweusi unaotokana na kuchoma msitu huvutia mvua. Wanaamini mawingu ya moshi hubadilika kuwa mawingu yanayoleta mvua siku chache baadaye. Ni desturi ya zamani ambayo bado inaaminiwa,” alisema.

Millicent Wangui, 79, alisema amesikia imani hiyo tangu akiwa mdogo.

“Miaka mingi iliyopita, vijana walikuwa wakichoma moto mashambani wakiamini utaleta mvua. Huenda hiyo ndiyo sababu baadhi yao wameanza kuchoma misitu,” alisema.

Lakini Bw Mkung alikataa imani hiyo akisema ni hatari.

“Hizo ni imani potofu. Kwa kweli zinaweza kuchelewesha mvua kutokana na gesi zinazotokana na moshi. Miti inajulikana kusaidia kuvuta mvua na hatuwezi kupata mvua zaidi kwa kuharibu misitu,” alisema.

Alisema wazima moto wanakabiliwa na hali ngumu kutokana na mimea mikavu na upepo mkali unaosambaza moto kwa kasi.

Kamanda wa KWS katika Kaunti ya Nyandarua Paul Wambugu alisema wazima moto kutoka Hifadhi ya Kitaifa ya Aberdare wametumwa kusaidia kuzima moto huo.

Afisa Mkuu wa Maji na Tabianchi wa Nyandarua Wachira Mugo alisema hali inazidi kuwa mbaya huku timu za kaunti zikishindwa kufikia baadhi ya maeneo yaliyoathiriwa kutokana na eneo kuwa na miinuko mikali.

“Serikali ya kaunti haina uwezo wa kutosha kudhibiti moto huu. Vifaa vyetu vya kuzima moto haviwezi kufika katika baadhi ya maeneo yaliyoathiriwa kutokana na hali ngumu ya ardhi. Wafanyakazi wetu wamelemewa,” alisema.

Alisema moto huo ulikuwa ukielekea katika maeneo muhimu ya vyanzo vya maji.

Aliomba msaada wa KFS, KWS na Jeshi la Ulinzi la Kenya (KDF).

Moto huo umechochewa na ukame wa muda mrefu ambao umefanya mimea kuwa mikavu sana pamoja na upepo mkali unaovuma upande wa magharibi wa msitu.

Gavana wa Nyandarua Kiarie Badilisha ameitaka serikali kuchukua hatua za haraka kuzuia moto huo usiharibu maeneo muhimu ya vyanzo vya maji.