Ruto aagiza maafisa wa polisi kuheshimu haki za binadamu
RAIS William Ruto amewataka maafisa wa usalama nchini kuzingatia haki za binadamu, uwajibikaji na utaalamu wanapotekeleza majukumu yao, huku serikali ikiendeleza mageuzi makubwa yanayolenga kuboresha huduma za polisi nchini.
Akizungumza Ijumaa katika hafla ya kufuzu kwa kundi la 59 la makurutu wa Huduma ya Polisi wa Utawala katika Chuo cha Kitaifa cha Polisi, Embakasi, Rais alisema kuwa mageuzi yanayoendelea katika Huduma ya Kitaifa ya Polisi yanalenga kujenga taasisi yenye uwajibikaji na inayowahudumia wananchi kwa ufanisi zaidi.
“Katiba inataka Huduma ya Kitaifa ya Polisi kudumisha taaluma na nidhamu, kuzuia ufisadi, kuzingatia uwazi na uwajibikaji, kuheshimu haki za binadamu na kudumisha imani ya wananchi,” alisema Rais Ruto.
Aliongeza kuwa misingi hiyo inapaswa kuongoza kila hatua ya maafisa wa polisi, kuanzia kukamatwa kwa washukiwa, uchunguzi wa makosa ya jinai, usimamizi wa mikusanyiko ya umma hadi mahusiano yao ya kila siku na wananchi.
Rais pia aliwakumbusha maafisa hao kuwa Katiba inalinda haki na uhuru mbalimbali ikiwemo uhuru wa kujieleza, kujiunga na vyama, kukusanyika, kuandamana na kushiriki shughuli za kisiasa, na kwamba polisi wana wajibu wa kulinda haki hizo.
“Katiba yetu pia inahakikisha uhuru wa kujieleza, kujumuika, kukusanyika, kuandamana na kushiriki kisiasa. Hizi ni haki muhimu katika mfumo wetu wa kidemokrasia na lazima ziheshimiwe na kulindwa,” alisema.
Rais alisema mageuzi ya polisi yanafanywa kwa manufaa ya umma na yanagharamiwa kwa fedha za walipa kodi, hivyo kila hatua katika mchakato huo lazima iwe wazi na iweze kuchunguzwa na wananchi.
“Mpango huu wote wa mageuzi unatekelezwa kwa maslahi ya umma na kwa kutumia rasilimali za umma,” alisema, akiongeza kuwa kila kipengele cha mageuzi hayo kinapaswa kuhimili uchunguzi wa wananchi.
Aliwaambia maafisa waliofuzu kuwa mafanikio ya mageuzi hayo hayatapimwa kwa sera, hotuba, sare mpya au vifaa vya kisasa pekee, bali kwa namna wananchi wa kawaida watakavyohudumiwa.
“Yatapimwa kwa kuangalia kama afisa anaitikia anapohitajika, anatekeleza sheria bila upendeleo, anakataa rushwa, analinda walio katika mazingira magumu, anaheshimu utu wa binadamu na anawatendea Wakenya wote kwa usawa mbele ya sheria,” alisema Rais.
Aliwataka maafisa hao kutekeleza majukumu yao kwa ujasiri lakini pia kwa kujizuia na kuonyesha utu.
“Hudumuni kwa ujasiri, lakini kwa kujizuia; tumieni mamlaka yenu, lakini kwa uwajibikaji; na tekelezeni sheria, lakini kwa ubinadamu,” alisema.
Kauli za Rais zilijiri huku Waziri wa Usalama wa Ndani na Utawala wa Kitaifa Kipchumba Murkomen akikanusha madai kwamba kuna vitengo vya polisi vinavyofanya kazi nje ya mamlaka ya Inspekta Jenerali wa Polisi Douglas Kanja.
Murkomen alisema madai hayo hayana ukweli na yanalenga kupotosha umma kuhusu muundo wa uongozi ndani ya Huduma ya Kitaifa ya Polisi.
“Wale wanaodai kwamba kuna vitengo ndani ya Huduma ya Kitaifa ya Polisi vinavyofanya kazi nje ya mamlaka ya Inspekta Jenerali ni wapotoshaji wa ukweli,” alisema.
Alisisitiza kuwa serikali itaendelea kuunga mkono uhuru wa Huduma ya Kitaifa ya Polisi na kuilinda dhidi ya ushawishi wa nje.
“Tutaendelea kuunga mkono uhuru wa NPS dhidi ya aina yoyote ya kuingiliwa kutoka nje,” alisema.
Murkomen alisema mageuzi yanayotekelezwa kwa sasa yanatokana na mapendekezo ya Jopokazi la Kitaifa kuhusu Mageuzi ya Polisi lililoongozwa na aliyekuwa Jaji Mkuu David Maraga.
Kwa mujibu wake, mageuzi hayo yanalenga kuunda huduma ya polisi yenye utaalamu, iliyoandaliwa vizuri, iliyo na vifaa vya kisasa na inayoweka maslahi ya wananchi mbele.
Miongoni mwa hatua zilizokwisha kutekelezwa ni kuboresha mitaala ya mafunzo ya polisi ili kuweka mkazo zaidi kwenye haki za binadamu, katiba na utawala wa sheria.
“Moja ya mambo yaliyofanyika ni kuboresha mtaala wa mafunzo. Sasa unajumuisha mafunzo kuhusu haki za binadamu, utawala wa kikatiba na utawala wa sheria,” alisema Murkomen.
Waziri huyo alisema serikali pia inawekeza pakubwa katika teknolojia na vifaa vya kisasa ili kuboresha operesheni za usalama na utoaji huduma kwa wananchi.
Rais alisema ustawi wa maafisa wa polisi umepewa kipaumbele katika mageuzi hayo. Alieleza kuwa serikali imekamilisha awamu tatu za nyongeza ya mishahara, hatua iliyoongeza mshahara wa msingi wa konstebo wa polisi kwa asilimia 36.