Ruto sasa atumia maafisa wa umma ‘kubembeleza’ Mlima
RAIS William Ruto sasa anawategemea makatibu wa Baraza la Mawaziri na maafisa wengine wa serikali kupeleka ujumbe wa serikali mashinani katika juhudi za kurejesha uungwaji mkono wa Mlima Kenya kabla ya uchaguzi mkuu wa 2027.
Mikakati hiyo inalenga kueleza wakazi mafanikio ya serikali ya Kenya Kwanza na kupunguza malalamishi kwamba eneo hilo limetengwa tangu aliyekuwa Naibu Rais Rigathi Gachagua kuondolewa mamlakani Oktoba 2024.
Rais Ruto amekiri kuwa serikali imekuwa na tatizo la kuwasilisha mafanikio yake kwa wananchi, hali ambayo amedai imeacha nafasi kwa taarifa potovu na kuchochea kutoridhika.
Maafisa wa serikali sasa wanafanya mikutano ya hadhara katika eneo la Mlima Kenya kueleza mipango ya serikali na kushughulikia malalamishi ya wananchi.
Wiki iliyopita, Katibu Mkuu wa Afya ya Umma Mary Muthoni alifanya baraza la wananchi Nyeri kupitia mpango wa Jamii Imara Mashinani, ambako alijibu maswali kuhusu afya, kilimo na miundombinu.
Bi Muthoni alisema serikali imegundua pengo la mawasiliano kuhusu Mamlaka ya Afya ya Jamii (SHA), akieleza kuwa wananchi wengi hawajui wanaweza kulipa michango yao kwa awamu kupitia mpango wa Lipa SHA Polepole.
Maafisa wengine waliohusika katika mikutano hiyo ni Waziri wa Utumishi wa Umma Geoffrey Ruku na Katibu Mkuu wa Kawi Alex Wachira.
Katika upande wa miundombinu, Mwenyekiti wa bodi ya Mamlaka ya Kitaifa ya Barabara Kuu (KeNHA), Winfrida Ngumi, alisema miradi ya barabara yenye thamani ya zaidi ya Sh46 bilioni imekamilika au inaendelea Nyeri.
Alisema pia barabara za Mau Mau, ambazo zilikuwa zimesimama, zimeanza tena baada ya wakandarasi kulipwa zaidi ya Sh5.5 bilioni.