MAONI: Hivi huyu Ndindi ni mpinzani wa Ruto au anamdhibiti tu Gachagua?
HATUA mpya ya kisiasa ya Mbunge wa Kiharu, Ndindi Nyoro, imezua kitendawili kipya katika siasa za kuelekea uchaguzi mkuu wa 2027.
Mwanasiasa huyo ambaye kwa muda mrefu alikuwa miongoni mwa watetezi wakuu wa Rais William Ruto ndani ya Kenya Kwanza, sasa anajijengea kao lake binafsi katika upinzani kupitia chama cha People’s Party of Kenya (PPK).
Hata hivyo, mabadiliko haya hayajatazamwa kama kuhama chama kwa kawaida.
Yanagusa masuala ya uaminifu wa kisiasa, tamaa ya madaraka na vita vya kuwania ushawishi katika ukanda wa Mlima Kenya.
Nyoro alikuwa sauti muhimu ya serikali akiwa Mwenyekiti wa Kamati ya Bajeti na Ugawaji wa Fedha ya Bunge la Kitaifa.
Alitetea sera na mipango ya Kenya Kwanza kwa nguvu, huku akimsifu Rais Ruto kama kiongozi aliyekuwa akileta maendeleo kwa kasi kubwa kuliko tawala zilizomtangulia.
Kwa hivyo, kugeuka kwake na sasa kushiriki kampeni za kumuondoa Ruto madarakani kunazua swali lisiloepukika: Ni nini hasa kilibadilika?
Nyoro anaeleza kwamba tofauti zake na Ruto zilianza wakati wa mchakato wa kumuondoa aliyekuwa naibu wa rais Rigathi Gachagua.
Anasema alikataa kuunga mkono mchakato huo. Bunge la Kitaifa lilipiga kura ya kumuondoa Gachagua mnamo Oktoba 8, 2024, kabla ya Seneti kuthibitisha kuondolewa kwake Oktoba 17.
Lakini swali kubwa ni: Kwa nini Nyoro ameunda PPK badala ya kujiunga na DCP au chama kingine katika mrengo wa upinzani?
DCP inajijenga kama nguzo kuu ya upinzani katika Mlima Kenya, huku Gachagua akijaribu kuunganisha eneo hilo kisiasa.
Nyoro, badala yake, anajenga kituo chake cha nguvu. Hii inazua dhana kwamba huenda hataki kuwa mwanajeshi katika safu ya Gachagua; anataka kuwa mchezaji huru mwenye uwezo wa kujinadi kama yeye tu.
Baadhi ya washirika wa Gachagua wanamshuku Nyoro kuwa anatumika kugawanya upinzani. Madai haya hayawezi kupuuzwa kabisa.
Chama kipya kinaweza kupanua upinzani kwa kuwapa wanasiasa nafasi mpya, lakini pia kinaweza kugawanya kura zinazompinga Rais Ruto.
Ikiwa hilo litatokea, serikali inaweza kunufaika hata kama Ndindi Nyoro hakuwa na nia hiyo.
Hapo ndipo wazo la kuwa kibaraka cha serikali linapopata nafasi katika mjadala wa kisiasa.
Huenda mkakati wake ni tofauti kabisa: kujenga wabunge, maseneta, magavana na madiwani wengi iwezekanavyo ili kuwa na nguvu ya kujadiliana wakati wa kuunda muungano wa 2027.
Kwa hivyo, PPK inaweza kuwa chombo cha kuunganisha au kuugawanya upinzani.
Je, Nyoro atamuunga mgombea mmoja wa upinzani hata kama hatakuwa yeye?
Je, PPK itaepuka kuweka wagombea ambao wanaweza kugawanya kura za upinzani katika maeneo muhimu?
Majibu ya maswali hayo yataamua iwapo Nyoro ni mjenzi au mbomoaji wa upinzani.
Kwa sasa, Ndindi Nyoro ni kituo kipya cha nguvu za kisiasa kinachoweza kubadilisha kabisa mizani ya siasa za Mlima Kenya.
Swali ni Je, Nyoro anajenga njia yake kuelekea ikuluni, au anajenga nguvu ya kisiasa ambayo itamruhusu kuwa mtu muhimu zaidi katika kuamua nani ataingia ikuluni mwaka 2027?