Habari za Kaunti

Rais amtaka Shahbal asiwanie ugavana Mombasa, asalie katika ujasiriamali

Na WINNIE ATIENO September 9th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

RAIS William Ruto amejitokeza waziwazi kumshawishi mfanyabiashara Suleiman Shahbal kuachana na azma ya kuwania ugavana wa Mombasa, akisema bwanyenye huyo anaweza kulitumikia taifa la Kenya vyema zaidi kwa kuunda ajira na kuwekeza katika biashara kuliko kujiingiza katika siasa za uchaguzi.

Akiongea katika Ikulu ya Nairobi, Dkt Ruto alisema alikuwa amemshauri binafsi Bw Shahbal dhidi ya kuwania ugavana.

“Nakumbuka nilimwambia Bw Shahbal kwamba najua unataka kuwania ugavana wa Mombasa, na nikamwambia kwamba ninapinga hilo. Nisamehe, ndugu yangu Shahbal, lakini wewe ni mjasiriamali mkubwa,” alisema Dkt Ruto.

Rais alikuwa akizungumza wakati wa kutiwa sahihi kwa makubaliano ya Sh12 bilioni kati ya GulfCap Group ya Bw Shahbal na kampuni ya kimataifa ya biashara za bandarini ya DP World kwa ajili ya kuendeleza Eneo Maalum la Kiuchumi lenye ukubwa wa ekari 535 eneo la Jomvu, Mombasa.

Mradi huo utawaleta pamoja wazalishaji, kampuni za usafirishaji mizigo, wauzaji wa bidhaa nje ya nchi na biashara nyingine karibu na Bandari ya Mombasa.

Bw Shahbal alisema kampuni kutoka Dubai, India, China, Vietnam na Ulaya tayari zimeonyesha nia ya kuanzisha shughuli katika eneo hilo, huku baadhi zikiiangalia Kenya kama kituo cha uzalishaji bidhaa kwa ajili ya masoko ya Afrika, Ulaya na Amerika.

Gavana wa Mombasa, Bw Abdulswamad Nassir aliipongeza hatua hiyo, akisema itatoa fursa kwa Mombasa kuzalisha bidhaa zilizokamilika zinazolenga masoko kote duniani.