Akili Mali

AKILIMALI: Mbinu tofauti za kuandaa nyama kuboresha biashara

September 9th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

MBINU mpya na za jadi za kupika na kuongeza nyama thamani zinaendelea kubadilisha sekta ya mifugo na nyama nchini, huku wafanyabiashara na wabunifu wakitumia teknolojia na maarifa mapya kuvutia walaji.

Haya yalijitokeza katika Maonyesho ya Kenya Meat Expo 2026 yaliyoandaliwa na Nation Media Group (NMG) kwa ushirikiano na Wizara ya Kilimo na Maendeleo ya Mifugo, pamoja na wadau wengine wa sekta hiyo.

Maonyesho hayo ambayo yalikuwa Makala ya Tano yalifanyika katika Ukumbi wa Kimataifa wa Mikutano wa Kenyatta (KICC), Nairobi, Agosti 26 hadi 28.

Wakulima, wasindikaji, wafanyabiashara, watafiti, mashirika muhimu kama vile ya kuuza nyama nje ya nchi, ya kifedha, ya malisho, wabunifu na mashabiki wa nyama walipata nafasi ya kujifunza mbinu tofauti za kupika na kuhifadhi nyama.

Miongoni mwa mbinu zilizovutia wengi ni uandaaji wa nyama kwa moshi.

Njia hii huhusisha kupika nyama kwa joto la chini kwa muda mrefu, huku moshi wa kuni ukiipa ladha ya kipekee.

Samuel Ndung’u, mwanzilishi wa Pikmaster Sam, alionyesha jinsi nyama ya brisket huandaliwa kwa kutumia kifaa maalumu cha kuvuta moshi.

Kwenye mahojiano na Akilimali, alisema nyama hiyo huchukua zaidi ya saa 12 kuiva kikamilifu.

“Tunapika polepole ili nyama isalie laini, yenye unyevu na ladha ya kipekee inayotokana na kuni tunazotumia,” anasema.

Ndung’u, ambaye aliacha kazi katika huduma ya polisi kuingia kwenye biashara ya nyama mwaka 2014, anasema mbinu hiyo imebadili mtazamo wa watu kuhusu nyama ya kuchoma.

Joshua Nzioka wa Camp David akiwa katika maonyesho ya nyama KICC Agosti 28, 2026. PICHA| DENNIS ONSONGO

Hata hivyo, anakiri kuwa gharama za uzalishaji ni kubwa kutokana na matumizi makubwa ya kuni, mafuta na wafanyakazi.

Kwa sasa, robo ya kuku katika biashara yake huuzwa kwa Sh400, kilo moja ya nyama ya kondoo kwa Sh1,800 huku hiyo iliyochomwa kwa moshi (brisket) ikiuzwa kwa Sh2,500 kwa kilo.

Mbali na uchomaji wa nyama kwa moshi, Martin King’ori wa Camp David Butchery, alionyesha teknolojia ya dry ageing, ambapo nyama huhifadhiwa katika mazingira yenye kiwango maalumu cha joto, unyevunyevu na mzunguko wa hewa kwa wiki kadhaa kabla ya kuuzwa au kupikwa.

Kulingana King’ori, mbinu hiyo huifanya nyama kuwa laini zaidi na kuongeza ladha yake.

“Maji hupungua polepole huku vimeng’enya vya asili vikivunja protini za misuli, jambo linaloboresha ubora wa nyama,” anasema.

Waziri wa Kilimo na Maendeleo ya Mifugo, Mutahi Kagwe, akizungumza wakati wa ufunguzi rasmi wa maonyesho hayo, alisema sekta ya nyama ina uwezo mkubwa kuunda ajira, kuongeza mapato ya wafugaji na kuimarisha mauzo ya bidhaa za Kenya nje ya nchi.

Alidokeza kwamba Kenya ilizalisha takriban tani 613,627 za nyama mwaka 2024 zenye thamani ya Sh397 bilioni.

“Nyama ya ng’ombe iliongoza kwa uzalishaji wa tani 260,000 zenye thamani ya karibu Sh160 bilioni,” Waziri Kagwe alielezea.

Hata hivyo, alisisitiza kuwa nchi haipaswi kutegemea nyama ya ng’ombe pekee, akitaja fursa zilizopo katika nyama ya mbuzi, kondoo, kuku, ngamia, nguruwe na sungura.

Waziri alisema Kenya inapaswa kuhamia kutoka kuuza mifugo hai hadi kuuza nyama, nyama iliyosindikwa na bidhaa zenye chapa maalumu ili kuongeza mapato na ajira nchini.

“Tunapouza mifugo hai nje ya nchi, tunakuwa pia tunauza nafasi za kazi ambazo zingepatikana hapa Kenya,” alisema.

Maonyesho hayo yalithibitisha kuwa sekta ya nyama inaendelea kupanuka na kwamba ubunifu katika usindikaji, upishi na masoko unaweza kufungulia vijana na wajasiriamali fursa mpya za kiuchumi na kazi.

Kauli mbiu ya hafla ya mwaka huu, 2026, ilikuwa kuimairisha ukuaji unaoweza kudumishwa pamoja na kukuza kizazi kijacho katika biashara ya nyama.